Hofu tele mauaji ya usiku yakitanda vijijini Kwale
WAKAZI wa vijiji vinavyopakana na misitu iliyo Mangawani, Kaunti ya Kwale, wanaishi kwa hofu ya mashambulio ya kihalifu ambayo yametanda kwa miaka kadha.
Wakazi hao wameeleza hofu kutokana na mfululizo wa mauaji ya kikatili na wizi unaodaiwa kufanywa na genge la wahalifu ambalo hufanya mashambulio usiku na kutoweka katika misitu inayozunguka vijiji hivyo.
Kulingana nao, washambuliaji hao hujitokeza kati ya saa mbili na saa tatu usiku, wakiwavamia watu wanaorejea nyumbani kutoka shughuli zao za kila siku.
Wakiwa wamejihami kwa mapanga, washambuliaji hao hudaiwa kuwajeruhi au kuwaua waathiriwa kwa haraka kabla ya kutoweka ghafla.
Bw Kisilu Mbai, 86, alisema kutokujulikana kwa wahusika wala nia yao ni jambo la kutisha sawa na mauaji yenyewe.
“Inashangaza kuwa wahusika hawawezi kupatikana. Tumekuwa tukisihi serikali itusaidie kuwapata, ili angalau tujue ni kina nani,” anasema.
Katika vijiji 17 vya Mangawani na maeneo jirani, baadhi ya wakazi wanaamini wahalifu hao hujificha katika misitu, huku wengine wakishuku kuwa ni watu kutoka maeneo ya nje wanaoingia vijijini kupanga mashambulizi kabla ya kutoroka.
Mauaji hayo pia yamehusishwa na migogoro ya kifamilia, mizozo ya urithi na uhasama wa muda mrefu wa kijamii, ingawa madai hayo hayajathibitishwa.
Bw Jacob Mwanzia anasema familia yake ilivunjika moyo baada ya nyanya yake kupatikana ameuawa.
“Hatuelewi nia ya washambulizi. Inaonekana wao hunuia tu kuua,” akasema.
Kulingana na wazee wa vijiji, mashambulizi hayo hujitokeza kwa vipindi vya miezi kadha.
Wakati huo, wazazi huwazuia watoto kutoka nje baada ya giza kuingia, makanisa hupunguza shughuli za usiku na waendesha bodaboda hufunga kazi mapema.
Mauaji hayo yameambatana na wizi wa mara kwa mara. Makanisa yameripotiwa kuvamiwa na kuibiwa vifaa vya matangazo, vyombo vya muziki, vifaa vya umeme na sadaka.
Pia, pikipiki, vifaa vya nyumbani na zana za kilimo zimeibwa.
Chifu Msaidizi wa Mangawani, Bw Salim Nzala anasema wamepokea ripoti za mauaji matatu tangu Desemba 2025, huku uchunguzi ukiashiria zaidi migogoro ya kifamilia.
“Visa vingi tulivyopokea viliwasilishwa kwa Idara ya Kuchunguza Uhalifu. Kilichosalia kwetu ni kuhakikisha kuna ushirikiano. Kwa hivyo wakazi wasilalamike kwamba serikali haijali, kwa sababu masuala yao yanashughulikiwa,” akasema.
Serikali imeanzisha kituo cha polisi Mangawani, imeongeza doria na kuandaa mikutano ya umma ili kuwahimiza wakazi kutoa taarifa.
Hata hivyo, wakazi wanataka hatua zaidi, wakisema misitu na barabara duni huwapa wahalifu nafasi ya kutoroka.
Kamanda wa Polisi wa eneo la Pwani, Bw Ali Nuno anasema hali ya usalama katika eneo zima kwa jumla imeimarika.