Habari

Idd: Wito viongozi wakome matamshi ya chuki na matusi uchaguzi wa 2027 ukikaribia

Na Na WAANDISHI WETU March 21st, 2026 Kusoma ni dakika: 2

VIONGOZI wa Kiislamu wameungana na viongozi wengine wa kidini kote nchini kukemea matamshi ya ukosefu wa maadili miongoni mwa wanasiasa, wakionya kuwa malumbano ya sasa ya kisiasa yanaweza kuhatarisha umoja wa taifa huku nchi ikielekea Uchaguzi Mkuu wa 2027.

Wakizungumza wakati wa maadhimisho ya Idd ul-Fitr katika maeneo mbalimbali ya nchi, viongozi hao waliwataka wanasiasa kudumisha heshima, maadili na mshikamano badala ya kueneza migawanyiko.

Katika jiji la Eldoret, mamia ya waumini walikusanyika katika uwanja wa Shule ya Msingi ya Uasin Gishu kwa swala ya Idd ambapo viongozi wa kidini waligeuza hafla hiyo kuwa jukwaa la kuonya tabaka la kisiasa dhidi ya matamshi ya chuki na matusi katika mikutano ya umma.

Imam wa Msikiti wa Eldoret Jamia, Sheikh Mohamed Hussein, alisema kurushiana maneno kati ya viongozi wa serikali na upinzani kumefikia kiwango kisichokubalika.

“Tunashuhudia mwenendo ambapo viongozi wanaopaswa kuwa walinzi wa maadili ya taifa wanajihusisha na matamshi yasiyofaa. Haya si matusi tu, bali pia yanaharibu malezi ya watoto wetu na kuweka mfano mbaya kwa vijana,” alisema.

Katika Kaunti ya Narok, Gavana Patrick Ntutu alitoa onyo kali kwa wanasiasa wanaotoa matamshi ya uchochezi akisema yeyote atakayepatikana akichochea vurugu wakati wa mikutano ya kisiasa atachukuliwa hatua kali za kisheria.

Akizungumza baada ya swala ya Idd katika uwanja wa William Ole Ntimama, alisema Narok imekuwa mfano wa utangamano wa jamii mbalimbali na viongozi hawapaswi kuharibu amani hiyo kwa matamshi ya kugawanya wananchi.

Viongozi wa Kiislamu katika eneo hilo wakiongozwa na Sheikh Salim pia waliwataka wanasiasa kuepuka matusi na kulinda amani kabla ya uchaguzi wa 2027.

Mwenyekiti wa Baraza Kuu la Waislamu tawi la Narok, Ali Juma, alisema ghasia si suluhu na akawasihi wananchi kudumisha utulivu kabla, wakati na baada ya uchaguzi.

Katika Kaunti ya Kakamega , Gavana Fernandes Barasa aliwataka viongozi wa upinzani kudumisha heshima kwa ofisi ya Rais na kuepuka mashambulizi ya mara kwa mara dhidi ya Rais William Ruto.

Akizungumza wakati wa sherehe za Idd katika Msikiti wa Jamia Shianda eneo la Mumias Mashariki, alisema ofisi ya rais ni ishara ya umoja wa taifa na haipaswi kudhalilishwa kwa siasa za kawaida.

Katika kaunti ya Mombasa, viongozi waliwataka Wakenya kutumia siku ya Idd kukuza upendo, msamaha na kusaidia walio katika mazingira magumu.

Waziri wa Madini na Uchumi wa Bahari Hassan Ali Joho aliwataka Waislamu kuendelea kusaidia mayatima, wajane na wagonjwa hata baada ya mwezi mtukufu wa Ramadhani.

Naye Gavana wa Mombasa Abdulswamad Shariff Nassir alisema sikukuu hiyo inapaswa kutumiwa kuimarisha mshikamano na kuacha tofauti za kisiasa.

Wakati huo huo, wakaazi kadhaa waliokuwa wakizuiliwa hospitalini kutokana na madeni ya matibabu waliruhusiwa kurejea nyumbani baada ya serikali ya kaunti kushirikiana na wafadhili kulipa bili zao.

Katika Kaunti ya Garissa, viongozi wa kidini wakiongozwa na Sheikh Abdullahi Salat pia waliwataka wanasiasa kupunguza maneno ya chuki na kuzingatia masuala ya maendeleo.

Walisisitiza kuwa viongozi wanapaswa kuwa mfano mzuri kwa vijana na kuonyesha heshima kwa wapinzani wao.
Viongozi hao kwa pamoja walikubaliana kwamba kudumisha amani, uvumilivu na mshikamano wa kitaifa ni muhimu kwa maendeleo ya Kenya hasa wakati taifa linaelekea kipindi kingine cha ushindani mkali wa kisiasa.