Habari

IEBC yasajili wapiga kura wapya 875,501 ndani ya wiki mbili

Na JUSTUS OCHIENG April 12th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

TAKRIBAN Wakenya 900,000 wamejisajili kuwa wapiga kura wapya ndani ya kipindi cha wiki mbili pekee, Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) imesema, huku ikiongeza kasi ya zoezi la Usajili Endelevu wa Wapiga Kura (ECVR) kote nchini kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.
Katika taarifa iliyotolewa Nairobi Ijumaa, Mwenyekiti wa IEBC Erastus Ethekon alisema jumla ya wapiga kura wapya 875,501 walijisajili kati ya Machi 30 na Aprili 9, 2026, akitaja ongezeko hilo kama “hatua ya kuvutia” katika ushiriki wa umma.
Takwimu za hivi punde zinaonyesha ongezeko kubwa ikilinganishwa na taarifa ya awali ya Aprili 3, 2026. Kulingana na IEBC, wapiga kura wapya 531,185 waliongezwa kati ya Aprili 3 na Aprili 9 pekee, ishara ya kasi inayoongezeka ambayo inaweza kubadilisha mwelekeo wa ushiriki wa wapiga kura kuelekea 2027.
Nairobi inaongoza kwa kusajili wapiga kura wapya 96,897, ikithibitisha nafasi yake kama kitovu kikuu cha ongezeko la wapiga kura nchini. Jiji hilo pia liliongoza kwa uhamishaji wa vituo vya kupiga kura kwa watu 10,309 na mabadiliko ya taarifa za wapiga kura 243.
Kiambu ilifuata kwa wapiga kura wapya 46,265, ikifuatiwa na Kakamega (40,110), Nakuru (32,559), Machakos (30,686) na Meru (27,502). Bungoma ilisajili 26,820 huku Turkana ikiwa na 25,012 na Kisii 24,785.
Katika ukanda wa pwani, Kilifi ilisajili wapiga kura 23,980, Mombasa 21,258 na Kwale 11,841, huku Lamu ikiwa na idadi ndogo zaidi ya 4,810.
Kaunti nyingine zilizo na usajili mdogo ni Isiolo (5,379), Mandera (7,337), Nyandarua (7,906) na Nyamira (8,146), hali inayoonyesha changamoto za mwamko katika maeneo ya mbali na yenye idadi ndogo ya watu.
Ripoti hiyo pia inaonyesha uhamaji mkubwa wa wapiga kura, hasa Kiambu (3,331), Nakuru (2,811), Kisii (2,839) na Mombasa (2,599), ambapo wengi wanahamisha vituo vyao vya kupiga kura.