Habari

IPOA yafichua njama ya polisi kuficha ukweli kuhusu kifo cha Ojwang’

Na CHARLES WASONGA June 12th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

MAMLAKA ya Kuchunguza Utendakazi wa Polisi (IPOA) imefichuliwa maseneta kile kinachoonekana kama njama ya polisi kuficha ukweli kuhusu chanzo cha kifo cha mwalimu-bloga Albert Ojwang’.

Akitoa ufichuzi huo kwenye ukumbi wa seneti Jumatano, Juni 11, 2025, Naibu Mwenyekiti wa mamlaka hiyo, inayochunguza kisa hicho, Anne Wanjiku alifuchua kuwa kamera za usalama (CCTV) katika kituo cha Central, Nairobi, alikozuiliwa mwendazake zilivurugwa.

“Maafisa wetu hawakuweza kubaini hali ya Ojwang’ alipowasilishwa katika kituo cha Central kwa sababu hawakupata picha za CCTV kuhusu matukio kituoni hapa alipoletwa. Hii ni kwa sababu kamera hizo za usalama zilikuwa zimevurugwa,” Bi Wanjiku akasema.

“Endapo CCTV katika kituo cha Centrali zilikuwa zikifanya kazi kama kawaida, zingeonyesha pia maafisa wa ambao walishughulikia na hata wale waliomtembelea akiwa kwenye seli,” afisa huyo, aliyemwakilisha mwenyekiti wa IPOA Isaack Hassan, akaongeza.

Bi Wanjiku aliandamana na Waziri wa Usalama Kipchumba Murkomen, Inspekta Jenerali wa Polisi Douglas Kanja na Naibu Mwenyekiti wa Tume ya Kitaifa ya Huduma za Polisi Edwin Kiprono Cheluget.

Bw Wanjiku alisema kuwa maafisa wa IPOA walipofika katika kituo cha Central Jumapili Juni 8, 2025, kuanza uchunguzi, walipata nyaza za kupitisha umeme kwa kamera ya CCTV zikiwa zimekatika.

“Baada ya maafisa wetu kuunganisha tena nyaya hizo, kamera hiyo ilianza kufanyakazi tena, kuonyesha kuwa zilikatizwa kimakusudi kuficha ushahidi,” Bi Wanjiku akasema.

Naibu Mwenyekiti huyo alisema uchunguzi wa IPOA kuhusu kisa hicho utakamilishwa baada ya siku 10.

“Baada ya hapo, faili ya uchunguzi itawasilishwa kwa afisi ya Mwendesha Mashtaka Mkuu (DPP),” Bi Wanjiku akaeleza.

Wakati huo huo, mwenyekiti IPOA Bw Hassan ameripotiwa akiungama kwamba hatua ya polisi kuvuruga eneo la tukio “ili kuficha ukweli” ni miongoni mwa changamoto ambazo mamlaka hiyo hukumbana nayo katika kazi yake.

“ Kazi yetu huwa ngumu pale maafisa wetu wanapofika katia eneo la tukio na kupata maafisa wa polisi wamelivuruga kimakusudi kuhujumu juhudi zetu za kuwapata wenzao na hatia. Vile vile, maafisa hao hudinda kutoa maelezo au ushahidi wowote wa kutusaidia katika kazi yetu,” Bw Hassan akasema kwenye mahojiano na Taifa Leo Jumanne.

Mwenyekiti huyo pia alitaja ukosefu wa fedha, maafisa wa kutosha wa uchunguzi na vifaa vya kazi kama changamoto zingine zinazokumba IPOA.

Lakini licha ya changamoto hizo, Rais William Ruto ameitaka mamlaka hiyo kuharakisha uchunguzi kuhusu kifo cha Ojwang’ ambaye pia ni mwalimu ili ukweli upatikane na “familia yake ipate haki.”

Katika kikoa cha Jumanne, maseneta pia walitaka kujua ni kwa nini mwenzake aliwekwa katika seli pekee yake baada ya kusafirishwa kutoka nyumbani kwao Homa Bay alikokamatwa Jumamosi, Juni 7, 2025