Habari

Jinsi vuguvugu la Linda Mwananchi linavyogeuka kuwa mwiba kwa Ruto

Na JUSTUS OCHIENG February 22nd, 2026 Kusoma ni dakika: 3

MZOZO ndani ya Chama cha Orange Democratic Movement (ODM) umezaa vuguvugu la Linda Mwananchi ambalo linaendelea kupanuka na kuwa mwiba kwa vinara wa Serikali Jumuishi Rais William Ruto na Dkt Oburu Oginga.
Kilichoanza kama malalamishi dhidi ya maamuzi ya ndani ya chama cha ODM, kimegeuka haraka kuwa vuguvugu pana la kisiasa linalounganisha ‘waasi’ wa chama hicho na viongozi vijana kutoka vyama vingine.
Katikati ya vita hivi vya kisiasa ni mapambano makali ya uongozi, yanayohusisha washirika wa kiongozi wa ODM, Dkt Oburu Oginga, dhidi ya kundi linalomuunga Katibu Mkuu wa ODM, na Seneta wa Nairobi, Edwin Sifuna.
Pande zote mbili zimekuwa zikilaumiana kwamba zinafadhiliwa na vigogo wa kisiasa wenye ushawishi. Jana, Linda Mwananchi lilikuwa Kakamega huku Linda Ground la Oburu likiwa Siaya.
Huku Oginga na mrengo wake wakidaiwa kufadhiliwa na Rais William Ruto, kambi ya Sifuna inakanusha madai kwamba inafadhiliwa na Rais (Mstaafu) Uhuru Kenyatta.
Viongozi wa Linda Mwananchi wanaonekana kukosesha usingizi Rais Ruto na Dkt Oburu ambao wametangaza mpango wa kushirikiana 2027 kiasi cha kumhusisha Bw Kenyatta.
Seneta wa Nairobi, Edwin Sifuna, anayechukuliwa kuwa kinara wa Linda Mwananchi aliteuliwa kuwa Katibu Mkuu wa ODM mnamo 2018 na kuchaguliwa Seneta wa Nairobi mwaka wa 2022.
Kuondolewa kwake kutoka wadhifa wa chama mnamo Februari 11, 2026, kulisababisha malumbano kisiasa. Hata hivyo, amepata afueni kutoka kwa Mahakama ya Kutatua Migogoro ya Vyama vya Kisiasa (PPDT), ambayo imezuia chama kutekeleza uamuzi wa kumvua wadhifa.
Mbunge wa Embakasi Mashariki, Babu Owino, ameibuka kama mtetezi mkuu wa Linda Mwananchi.
Owino alitamba akiwa Mwenyekiti wa Wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Nairobi (SONU), akajijengea jina kupitia uanaharakati wa wanafunzi kabla ya kujiunga na siasa mwaka 2017.
Gavana wa Siaya, James Orengo, analeta kumbukumbu za kihistoria kwenye kampeni ya Linda Mwananchi.
Orengo alikuwa mstari wa mbele katika kupigania demokrasia na kupinga utawala wa chama kimoja katika miaka ya 1980.
Amekuwa Mbunge, Seneta, Mgombea Urais na Waziri katika serikali ya marehemu Mwai Kibaki.
Seneta wa Vihiga, Godfrey Osotsi, mtaalamu wa sayansi ya kompyuta na ana shahada za juu katika biashara na teknolojia. Osotsi alijiunga na ODM na sasa ni Naibu Kiongozi wa chama.
Osotsi amekuwa na msimamo kuhusu kufuata kanuni za chama, na amesisitiza kuwa mgogoro huu ni kuhusu kufuata sheria za chama na si vita vya madaraka.
Mbunge wa Saboti, Caleb Amisi, ni mmoja wa wabunge vijana wanaoibuka katika siasa za Kenya. Amisi amekuwa akisisitiza haja ya mabadiliko ya kisiasa na amepinga vikali muungano wowote kati ya ODM na UDA unaoungwa mkono na Rais Ruto.
Mwanachama wa Bunge la Mashariki mwa Afrika (EALA), Winnie Odinga, ambaye ni binti wa aliyekuwa kiongozi wa ODM Raila Odinga, ameongeza uzito wa kihisia na kihistoria katika vuguvugu hili. Winnie amekuwa akirai viongozi wa ODM kuendeleza mapenzi ya baba yake kwa demokrasia ya ndani na uwazi.
Seneta wa Kisii, Richard Onyonka na Anthony Kibagendi, Mbunge wa Kitutu Chache Kusini, pia wamejitokeza kama viongozi muhimu katika vuguvugu hili.
 Mbunge wa Kabuchai, Majimbo Kalasinga, na Mbunge wa Suba Kusini, Caroli Omondi, wamejiunga na kampeni ya Linda Mwananchi. Kalasinga, ameungana na Sifuna na kuhakikisha kuwa haki za wananchi zinapewa kipaumbele dhidi ya viongozi wa kisiasa. Omondi, ambaye alikuwa akishirikiana na serikali ya Ruto, amehamia upande wa upinzani kutokana na mabadiliko ya kisiasa katika kaunti yake.
Wabunge Joshua Kimilu ( Kaiti)Jack Wamboka (Mbunge wa Bumula), Patrick Makau (Mbunge wa Mavoko), Wilberforce Oundo (Mbunge wa Funyula) na Julius Mawathe (Embakasi Kusini) pia ni majina maarufu yanayohusishwa na Linda Mwananchi. Wamboka amekuwa akipinga utawala wa sasa, huku Makau na Oundo wakipigania haki za wananchi na kuhakikisha maendeleo ya msingi yanaendelea katika maeneo yao.
Mbunge wa Kitutu Masaba, Clive Ombane, na Mbunge wa Wundanyi, Danson Mwashako, ni majina mengine yanayohusishwa na Linda Mwananchi.
Wengine wanaotoa mchango mkubwa katika mikutano ya Linda Mwananchi ni Barongo Obadiah, Okong’o Omogeni, na Pauline Njoroge.