Habari

Kalonzo kuzuru Amerika uchaguzi mkuu ukikaribia

Na NDUBI MOTURI February 1st, 2026 Kusoma ni dakika: 3

KIONGOZI wa Wiper, Kalonzo Musyoka, anatarajiwa kusafiri nje ya nchi Jumanne kwenda Amerika katika ziara inayolenga, miongoni mwa mambo mengine, kuimarisha taswira yake kimataifa.
Ziara hiyo ya hali ya juu, pia inatarajiwa kupiga jeki kampeni zake kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027, ikizingatiwa kuwa fedha zinatarajiwa kutekeleza nafasi kubwa katika uchaguzi na pia ataitumia kuvutia dunia katika siasa za ndani wakati ambao serikali inalaumiwa kwa kukandamiza uhuru wa kiraia.
Kama sehemu ya kujijenga upya ndani ya muungano wa upinzani, kiongozi wa DCP Rigathi Gachagua, ambaye ni mshirika mkuu wa Bw Musyoka alizuru Amerika na kukutana na Wakenya wanaoishi ughaibuni.
Wasaidizi wa Bw Musyoka wanasema atatumia ziara hiyo kupigia debe muungano wa upinzani huku kinyang’anyiro cha 2027 kikizidi kupamba moto.
Bw Musyoka anatarajiwa kuwasili Washington, kuhudhuria Mkutano wa Kitaifa wa Maombi katika ukumbi wa Capitol Rotunda mnamo Februari 5.
Hafla hiyo ya kimataifa huhudhuriwa na zaidi ya washiriki 3,000 walioalikwa, wakiwemo wakuu wa nchi, wanadiplomasia wakuu, watunga sera na viongozi wa kidini kutoka kote duniani.
Kwa mujibu wa wasaidizi wake, kualikwa kwake kunathibitisha ushawishi wake wa muda mrefu ndani ya mitandao ya kisiasa ya Kenya na kimataifa.
Katika ziara hiyo, Bw Musyoka pia anatarajiwa kukutana na Wakenya wanaoishi Maryland na Virginia.
Aidha, atafanya mikutano kadhaa na maafisa wa serikali ya Amerika na wataalamu wa Kenya walioko ughaibuni kuzungumia masuala ya utawala, siasa za kikanda na kupigia debe azma yake ya 2027.
Kwa mujibu wa vyanzo vinavyofahamu ratiba yake, Makamu Rais huyo wa zamani pia amepangiwa kukutana na maafisa kutoka Ikulu ya Amerika pamoja na watu wanaohusishwa kisiasa ya Rais Donald Trump.
Mikutano hiyo inalenga kuimarisha mawasiliano ya kisiasa ya ngazi ya juu na kupanua uungwaji mkono kimataifa 2027 inavyokaribia.
Endapo ataamua kuwania urais, anatarajiwa kutegemea uhusiano huo kufadhili kampeni zake.
Seneta wa Makueni Daniel Maanzo alisema ziara ya Bw Musyoka Washington imejikita kimkakati kwenye mitandao ya kimataifa ambayo Bw Musyoka alijenga kwa miaka mingi.
“Mheshimiwa Kalonzo Musyoka ana marafiki wengi Amerika. Alikuwa sehemu ya timu iliyoanzisha Maombi ya Kitaifa mwaka 2003. Atatumia fursa hiyo kufufua mahusiano na marafiki wake wa zamani, hususan wanadiplomasia na wakuu wa nchi,” alisema Bw Maanzo.
 Alieleza kuwa mkutano huo ni mkusanyiko wa kidiplomasia usioweza kulinganishwa na majukwaa mengi ya kisiasa.
“Hafla hiyo ya maombi ya kitaifa huwaleta pamoja zaidi ya wageni 3,000 kutoka duniani kote. Kwa mgombea urais, uwezo wa kujenga mahusiano na mataifa mengine ni muhimu. Mheshimiwa Musyoka pia atatumia fursa hiyo kurai marafiki wa kimataifa kuunga mkono azma yake ya kuleta mabadiliko na kubadilisha Kenya endapo atachaguliwa Rais mwaka 2027,” aliongeza.
Bw Maanzo pia alibainisha kuwa Bw Musyoka atakutana na viongozi na wanadiplomasia wa Afrika katika vikao maalum vya kieneo.
“Kutakuwa na vikao vya Afrika ambapo wakuu wa nchi na wanadiplomasia hukutana. Hiki kitakuwa kikao kizuri kwa Musyoka kukutana nao na kupanua mtandao wake,” alisema.
Baadhi ya wakuu wa nchi za Afrika wanaotarajiwa kuhudhuria ni Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) Félix Tshisekedi na Rais wa Guinea Mamadi Doumbouya.
 Bw Musyoka pia anatarajiwa kukutana na Seneta Chris Coons wa Delaware, ambaye ni mhusika muhimu katika diplomasia ya kikanda na aliyesaidia kupatanisha Rais Uhuru Kenyatta na kiongozi wa upinzani Raila Odinga mwaka wa 2018.
Kabla ya ziara hiyo, leo atafanya mazungumzo ya moja kwa moja kwa njia ya mtandao na Wakenya wanaoishi ughaibuni.
Atatumia jukwaa hilo kujadili masuala ya kitaifa, kueleza misimamo ya sera za upinzani na kujibu changamoto zinazowakumba raia wanaoishi nje ya nchi.
Ziara yake inajiri wakati ambapo viongozi wa upinzani wanazidi kugeuza Amerika kuwa uwanja wa kisiasa. Aliyekuwa waziri wa Usalama wa Ndani Fred Matiang’i amefanya mikutano na wataalamu wa Kenya katika miji mikubwa ya Amerika, huku kiongozi wa People’s Liberation Party Martha Karua naye akizuru nchi hiyo mwaka jana.
Aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua alikamilisha ziara ya mwezi mmoja Amerika alikohutubia mikutano ya hadhara majimbo ya Dallas, California, Seattle, Boston na Baltimore.