Eritrea yadaiwa kusafirisha silaha kwa vikosi vya serikali Sudan
INADAIWA kuwa Eritrea sasa inatumika kama lango jipya la kusafirisha silaha kwa vikosi vya serikali yenye makao yake mjini Port Sudan.
Haya yanajiri huku mapigano yakiendela kati ya Wanajeshi wa Sudan na kundi la RSF katika maeneo ya kaskazini na mashariki mwa mji mkuu wa Darfur.
Hii ni baada ya kufichuliwa kuwa silaha mbalimbali za kivita ziliwasili nchini humo, hatua inayoaminika itasaidia kukabiliana na kikundi cha RFS.
Hatua hii inaonekana kuwa itafanya mapigano nchini humo kuendelea kuwa mbaya Zaidi.
Haya yanajiri baada ya ripoti kuibuka kwamba mkuu wa zamani wa ujasusi wa Sudan Salah Gosh alitembelea Eritrea mnamo Mei 16 mwaka huu na kukutana na Rais Isaias Afwerki.
Wawili hao waliripotiwa kukubaliana kuwa Asmara itakuwa mstari wa mbele kwa ununuzi wa silaha kwa niaba ya vikosi vya Bandari ya Sudan na wanamgambo washirika, kwa kutumia bandari za Eritrea kama sehemu za kupitisha silaha hizo.
Salah Gosh anajulikana sana kwa udalali wa mikataba ya silaha na ulanguzi wa silaha.
Mara nyingi anarejelewa kama “mtu mwenye nguvu Sudan,” kwani ana historia ndefu ya utumishi chini ya rais aliyeondolewa madarakani Omar al-Bashir.
Tangu kuanguka kwa utawala huo mnamo 2019, ushawishi wake umeongezeka kupitia muungano wake na vikosi vya Jenerali Abdel Fattah al-Burhan, ambapo inadaiwa ana jukumu muhimu katika kuwezesha ulaguzi wa silaha.
Ripoti zinaonyesha kuwa ndege zisizo na rubani za Uturuki na Iran zinawasili Port Sudan kupitia uwanja wa ndege wa Asmara.
Hizi ni pamoja na ndege zisizo na rubani za Bayraktar TB2 za Uturuki na zile kutoka Iran Mohajer-6 zenye uwezo wa kubeba mabomu. Hii inafuatia ushahidi unaoongezeka wa msaada kutoka Ankara na Tehran kwa vikosi vya Al-Burhan.
Tangu kuzuka kwa vita nchini Sudan mwezi Aprili 2023, Eritrea imekuwa na jukumu muhimu katika kusambaza vifaa vya kijeshi.
Ushirikiano unaokua kati ya mamlaka ya Eritrea na serikali ya Sudan unaenea zaidi ya usambazaji wa silaha na matumizi ya bandari. Ripoti zimeashiria maendeleo ya haraka ya kijeshi na kisiasa kati ya pande hizo mbili. Hasa, vikosi vya Al-Burhan viliripotiwa kuhamisha ndege za kivita hadi Asmara kama hatua ya tahadhari kufuatia mfululizo wa mashambulio ya ndege zisizo na rubani kulenga maeneo ya kiraia na kijeshi huko Port Sudan tangu Mei 4.
Uhusiano kati ya Asmara na serikali ya Bandari ya Sudan umeongezeka kwa kiasi kikubwa katika kipindi cha miaka miwili ya mzozo. Al-Burhan mwenyewe amefanya ziara nyingi nchini Eritrea, hivi majuzi zaidi ikiwa ya Aprili 2025.
Ripoti nyingine zinasema kuwa vikosi vya Bandari ya Sudan vimejenga maeneo maalum ndani ya kambi nyingi za kijeshi ili kulinda silaha na ndege zisizo na rubani. Hizi ni pamoja na mifumo ya hali ya juu ya rada na vifaa vya ulinzi, vinavyokusudiwa kukabiliana na mashambulizi ya ndege zisizo na rubani za RSF.
Haya yanajiri huku mataifa mbalimbali yakitoa wito mapigano hayo yamalizwe haraka.