Gabon yazima mitandao ‘kuokoa’ nchi
LIBREVILLE, GABON
GABON jana ilisitisha matumizi ya baadhi ya mitandao ya kijamii ikisema machapisho yao yanahatarisha usalama na uthabiti wa taifa hilo.
Mamlaka ya Mawasiliano ya Gabon (HAC) iliamrisha kusitishwa kwa matumizi ya mitandao hiyo ya kijamii kwa muda usiojulikana.
Hata hivyo, haikutaja moja kwa moja mitandao ambayo iliathirika na uamuzi huo.
NetBlock ambayo hudhibiti matumizi ya Intaneti ilisema kuwa Meta, You Tube na TikTok zilikuwa zikidhibitiwa na serikali ya Gabon.
Hata hivyo, Facebook, Instagram na X bado zilikuwa zikifanya kazi kufikia Jumatano mchana.
“Mitandao imekuwa ikitumiwa na wanaharakati kueneza matusi na kuchapisha habari ambazo zinahatarisha usalama wa taifa,” ikasema HAC.
Serikali haikuweka wazi chapisho ambalo limefanya wadhibiti na kusitisha matumizi ya baadhi ya mitandao kwa muda.
“Kusitisha matumizi ya mitandao enzi hizi hakutasaidia chochote kwa sababu changamoto kama ukosefu wa ajira na nyingine bado zipo. Serikali ingeweka juhudi katika kuzitatua changamoto hizi,” akasema Mwanaharakati Nicaise Moulombi.
“Mitandao si majukwaa ya burudani kama zamani, sasa inatumika kufanya kazi, kuyatoa maoni, uvumbuzi, biashara na kupigania haki,” akaongeza.
Rais wa Gabon Brice Oligui Nguema amekuwa akikabiliwa na wakati mgumu kuongoza nchi hiyo tangu atwae mamlaka kupitia mapinduzi mnamo Agosti 2023.
Mapinduzi hayo yalitamatisha uongozi wa nusu mwongo wa Rais wa zamani Ali Bongo na familia yake.
Taifa hilo ambalo linafahamika kutokana na uzalishaji wa mafuta kwa sasa linaandamwa na zigo kubwa la madeni. Raia wake milioni 2.5 nao ni maskini na hutegemea tu chakula kutoka nje ya nchi.