• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 7:50 PM
Huenda aina mpya ya corona ikazimisha uchumi wa dunia

Huenda aina mpya ya corona ikazimisha uchumi wa dunia

WANDERI KAMAU Na BENSON MATHEKA

HALI ya wasiwasi imetanda duniani kufuatia kuchipuka kwa aina mpya ya virusi vya corona, ambavyo vimetajwa kuwa hatari zaidi na wataalamu kuliko ile ambato imekuwa ikihangaisha ulimwengu kwa miezi kumi na moja sasa.

Aina hiyo iligunduliwa kwanza nchini Uingereza siku kadhaa zilizopita na wanasayansi wanasema kwamba, inaenea kwa haraka na kulemea vijana tofauti na iliyoanza kutetemesha ulimwengu kuanzia Desemba mwaka jana na kuathiri zaidi watu wa umri mkubwa.

Tayari, aina hiyo mpya ya corona imeguduliwa katika nchi nyingi za bara Ulaya. Mnamo Jumatatu, Kituo cha Kudhibiti Magonjwa barani Ulaya (ECDC) kilisema kuwa, aina hiyo ya virusi pia imegunduliwa katika nchi za Australia, Iceland, Denmark, Italia, Uholanzi na Ubelgiji.

Virusi vipya vya corona, pia viligunduliwa Afrika Kusini, ingawa serikali ya taifa hilo imesema ni tofaut nai vilivyopatikana Uingereza.Hata hivyo, serikali nchini humo ilitaja aina hiyo mpya ya virusi kuwa chanzo kikuu cha kuongezeka kwa maambukizi miongoni mwa vijana katika siku za hivi karibuni.

Tayari, nchi kadhaa barani Ulaya na Asia zimesimamisha safari za ndege kwenda Uingereza ili kudhibiti maambukizi ya virusi hivyo vipya.Jana, waziri wa afya Mutahi Kagwe alisema, serikali inafuatilia hali kabla ya kuamua kusimamisha safari za ndege kutoka nchi hiyo.

Wizara ya Mashauri ya Uingereza nayo imetoa tahadhari kwa wale wanaopanga kuingia ama kuondoka nchini humo, kuzingatia masharti mapya yaliyotolewa na serikali kudhibiti maambukizi.

“Safari za kimataifa kuingia ama kuondoka Uingereza zimewekewa masharti makali. Nchi zimeanza kufunga mipaka yao na huenda zikatangaza masharti mapya kighafla. Tafadhali shauriana na shirika la ndege unalopanga kusafiria ili kuelewa hali ilivyo,” ikasema wizara hiyo.

Mnamo wikendi, wataalamu nchini Uingereza walitaja virusi hivyo kuwa hatari sana, ambapo vinasambazwa haraka mara saba zaidi ya virusi vya sasa.

Mchipuko huo pia unaonekana kufifisha matumaini ya kupatikana kwa chanjo mpya, hasa baada ya watu waliopewa chanjo hiyo katika nchi kadhaa kuripotiwa kupata matatizo tofauti kiafya.

Haya yanajiri wakati huduma za matibabu zimesambaratika nchini Kenya kutokana na mgomo wa madaktari na wahudumu wa afya.Hofu imezuka kuwa huenda Kenya ikawa mwathiriwa mkuu wa wimbi hilo jipya la maambukizi, kwani ni mshirika wa karibu wa Uingereza na mataifa mengine ya Ulaya.

Kulingana na waziri msaidizi wa Afya Dkt Mercy Mwangangi, virusi hivyo vipya ni changamoto kwa juhudi za kukabiliana na janga ambalo limeathiri sekta ya afya na uchumi.

“Tunafuatilia kwa karibu hali ilivyo Uingereza baada ya kugunduliwa kwa aina mpya ya virusi ambavyo vinaathiri watu wa umri mdogo,” alisema Dkt Mwangangi jana asubuhi.

Mataifa ya Ufaransa, Ujerumani, Italia, Denmark, Uswisi, Ireland, Austria, Ureno, Sweden, Ubelgiji, Bulgaria, Hong Kong, Israeli, Iran, Croatia, Argentina, El Salvador, Chile, Morocco na Kuwait tayari yamepiga marufuku ndege kutoka nchini Uingereza.

Saudi Arabia imesitisha safari zote za kimataifa kwa kipindi cha wiki moja kufuatia kuongezeka kwa visa vya maambukizi ya corona nchini humo.

Wataalamu wanasema virusi hivyo vinajibadilisha mara kwa mara.Wataalamu sasa wanahofia kuwa chanjo inayoendelea kutolewa kuzuia virusi vya corona nchini humo huenda ikakosa kufanya kazi.

Waziri wa Afya wa Uingereza, Matt Hancock alisema kuwa, virusi hivyo vipya vya corona vinasambaa kwa kasi ya juu na huenda serikali ikalemewa.

You can share this post!

Kalembe Ndile kumpa Wambua ekari mbili za shamba wiki hii

2020: Demokrasia ilivyodorora Afrika kupitia chaguzi...