ICC yakemea Amerika kwa kuwawekea majaji wake vikwazo
AMSTERDAM, UHOLANZI
MAHAKAMA ya Kimataifa ya Uhalifu (ICC) Ijumaa ilitangaza kukerwa na hatua ya serikali ya Rais Donald Trump kuwekea vikwazo majaji wanne wakuu wa korti hiyo.
“Hizi ni juhudi za kutatiza ICC isijisimamie na isitekeleze majukumu yake bila kuingiliwa,” ikasema taarifa ya ngazi ya juu ya uongozi wa ICC.
Waziri wa Masuala ya Nje wa Amerika Marco Rubio alisema kuwa kuwekwa kwa vikwazo hivyo kunatokana na kile ilichokitaja kuwa majaji hao wanne kulenga Amerika na Israeli kwenye maamuzi yao.
Majaji hao wanne ni Solomy Balungi wa Uganda, Luz del Carmen Ibanez wa Peru, Reine Adelaide Sophie Alapini-Gansou wa Benin na Beti Hohler wa Slovenia.
Trump aliagiza baraza lake la mawaziri liandae mwongozo wa kuwekea ICC vikwazo baada ya mahakama hiyo kutoa amri ya kukamatwa kwa Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu pamoja na aliyekuwa Waziri wa Ulinzi Yoav Gallant.
Netanyahu na Gallant wanashutumiwa kwa kusimamia mauaji ambayo yamekuwa yakiendelea ukanda wa Gaza hasa yanayolenga wapiganaji wa Hamas.
Majaji wawili kwenye orodha hiyo walitoa amri ya kukamatwa kwa Netanyahu na Gallant nao wengine wawili walikubali ICC iendeleze uchunguzi dhidi ya dhuluma zilizodaiwa kutendwa na Amerika kule Afghanistan.
“Majaji hawa wamekuwa wakilenga Amerika kupitia maamuzi yao kwenye ICC, mahakama inayotumika tu kulenga mataifa na watu binafsi. ICC imekuwa ikitumia mamlaka yake vibaya na kuingilia uhuru wa mataifa pamoja na kutaka kudhibiti na kuvuruga asasi zao za kiusalama,” akasema Rubio.