Iran yaanza kumuaga Ayatollah mwanawe Mojtaba Khamenei akiwa pazuri kumrithi
TEHRAN, IRAN
IRAN Jumatano, Machi 4, 2026 ilianza hafla ya siku tatu ya kumuaga Kiongozi wa Kidini Ayatollah Ali Khamenei ambaye aliuawa Jumamosi akiwa na umri wa miaka 86.
Khamenei aliuawa kupitia mashambulizi ya angani yaliyotekelezwa na Amerika na Israeli.
Maelfu ya raia wa Iran Jumatano walianza kumiminika Tehran kumuaga kiongozi huyo ambaye amekuwa madarakani kutoka 1989.
Alichukua uongozi kutoka kwa Ayatollah Ruhollah Khomeini ambaye alikuwa mwanzishili wa Jamuhuri ya Kiislamu ya Iran mnamo 1979.
Khamenei pia alihudumu kama rais wa Iran kutoka 1981-1989.
Ayatollah Khamenei alikita utawala wake kwa msingi wa chuki dhidi ya Amerika huku nyumbani raia wakilalamika alikuwa akiongoza kwa njia ya udikteta.
Hojjatoleslam Mahmoudi, Mkuu wa Baraza la Kiislamu la Iran alisema Khamenei ataagwa kwa siku tatu na msafara wa mazishi yake utatangazwa baadaye.
Mahmoudi alisema umma utaruhusiwa kuutazama mwili wa Khamenei na kumpa heshima zao za mwisho kwa siku hizo tatu.
Raia walianza kumiminika katika ukumbi wa maombi ya Imam Khomeini kumuaga Khamenei.
“Ukumbi huo utakuwa ukiwapokea wageni na raia wa Iran ambao watakuwa wamekuja kumuaga kiongozi wetu wa kidini na kuonyesha Amerika kuwa Iran bado ni taifa imara na halitawainamia,” akasema Mahmoudi.
Mojtaba Khamenei, mwanawe Ayatollah Ali Khamenei anaonekana kuwa pazuri kurithi nafasi hiyo kutoka kwa babake na kuwa kiongozi mpya wa kidini wa Iran.
Hata hivyo, viongozi wa kidini wameashiria kuwa bado hawatatangaza atakayejaza nafasi hiyo kwa sababu wanahofia atalengwa na Amerika na Israeli.
Iran imeendeleza maasi dhidi ya Amerika kwa kurusha droni kwenye kambi za kijeshi za Amerika katika nchi hizo za ukanda wa Ghuba.
Mashambulizi ya droni na angani ya Iran yamevuruga uchukuzi wa ndege kwenye anga za ukanda wa Mashariki ya Kati.
Mashirika ya Ndege ya Qatar Airways, Emirates na Etihad yamethibitisha kuwa shughuli zao za uchukuzi bado zimesimamishwa kutokana na anga kutokuwa salama.
Mnamo Jumanne usiku, droni ya Iran ilipiga eneo la maegesho katika ubalozi wa Amerika Dubai na kusababisha moto na moshi mkubwa.
Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Amerika Marco Rubio alisema wafanyakazi wote kwenye ubalozi huo walikuwa salama.
Pia Iran iliendelea kuonyesha weledi wake Jumanne kwa kupiga ubalozi wa Amerika Riyadh vita hivyo vikiendelea.
Amerika imelazimika kufunga ubalozi wake Saudi Arabia, Kuwait na Lebanon na kuwashauri raia wake waondoke mataifa 14 ya Ukanda wa Mashariki ya Kati.
Haya yanajiri siku moja tu baada ya kamanda mmoja katika Kikosi cha Walinzi wa Mapinduzi cha Iran (IRGC) kusema kuwa Mkondo-Bahari wa Hormuz ungefungwa na kuonya kwamba chombo chochote kitakachojaribu kupita eneo hilo kitashambuliwa.
“Mkondo wa Hormuz umefungwa. Ikiwa mtu yeyote atajaribu kupitia hapo, mashujaa wa Walinzi wa Mapinduzi na jeshi la majini watateketeza meli hizo,” Ebrahim Jabari, mshauri mkuu wa kamanda mkuu wa IRGC, alisema.
Tehran sasa inalenga miundombinu muhimu wa kuzalisha nishati duniani kama sehemu ya kulipiza kisasi kwa mashambulizi ya Israeli na Amerika yaliyoanza Jumamosi na kusababisha kifo cha Kiongozi Mkuu wa Iran Ayatollah Ali Khamenei na maafisa wengine wakuu.
Rais Donald Trump ameapa kulipiza kisasi kwa uamuzi wake wa kuushambulia ubalozi wa nchi yake na kwa mauaji ya wanajeshi 6.