Israel yadai imemuua mkuu wa jeshi, Mojtaba akisema vita lazima viendelee
JERUSALEM, ISRAEL
WAZIRI wa Ulinzi wa Israel Katz Jumanne, Machi 17, 2026 alidai kuwa wanajeshi wa Amerika-Israel walimuua mkuu wa jeshi la Iran na mkuu wa wapiganaji wa Basij kwenye misururu ya mashambulizi ya angani Jumatatu siku.
Iran nayo haiwaachi mataifa ya Ghuba yenye kambi za kijeshi za Amerika yapumue, na jana iliendelea kuyashambulia huku bei ya mafuta pia ikipanda.
Katz kupitia taarifa alisema alikuwa amefahamishwa kuwa Mkuu wa Jeshi wa Iran Ali Larijani alikuwa ameuawa.
Vyombo vya habari Iran navyo vilichapisha karatasi iliyokuwa imeandikwa na Larijani kuwaenzi manahodha wa meli za Iran waliokuwa wameuawa na Amerika.
Mazishi ya manahodha hao yalikuwa yafanyike Jumanne.
Larijani iwapo kweli ameuawa, atakuwa afisa wa ngazi ya juu zaidi serikali ya Iran kuuawa na Israel-Amerika baada ya mauti ya Kiongozi Mkuu Ayatollah Khamenei mnamo Februari 28.
Pia Katz alisema Gholamreza Soleimani, Kamanda wa wapiganaji wa Basij alikuwa ameuawa. Wapiganaji wa Basij huwa wanaegemea Iran na wanadhibitiwa na wanajeshi wa Jamuhuri ya Kiislamu ya Iran.
Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu kupitia afisi yake, alisema kuwa kiongozi huyo alikuwa ameamrisha viongozi wote wa ngazi ya juu wa Iran wauawe.
Vita vya Amerika-Israel dhidi ya Iran vipo katika wiki yake ya tatu ambapo zaidi ya watu 2,000 wameuawa na havionekani kama vitaisha hivi karibuni.
Iran imefunga Mkondo wa Hormuz ambao asilimia 20 ya mafuta ulimwenguni hupitia huku washirika wa Amerika wakikataa kuingilia vita hivyo, kufungua eneo hilo.
Iran bado inaendelea kurushia droni Israel nao wanajeshi wa Israel wakilenga miundomsingi ya serikali ya Iran.
Pia Israel inawalenga wapiganaji wa Hezbollah jijini Beirut na kusema ishachora mwongozo wa wiki tatu wa kuendelea kushambulia Iran.
Haya yanafanyika wakati ambapo Kiongozi Mkuu wa Iran Mojtaba Khamenei amekataa mapendekezo ya kusitisha vita kati ya Iran na Amerika.
Afisa mmoja wa serikali ya Iran alisema kuwa Mojtaba alifikishiwa pendekezo hilo na wawakilishi wa mataifa mawili patanishi lakini akakataa.
Kwa mujibu wa afisa huyo, Mojtaba alisema kuwa huu si wakati mwafaka wa kusitisha vita hivyo.
“Alisema vita vitaisha tu baada ya Amerika na Israel kumalizwa kisha kuwe na msamaha na raia wa Iran walipwe fidia,” akasema afisa huyo.
Duru zinaarifu pia Rais wa Amerika Donald Trump amesambaratisha jaribio la baadhi ya mataifa ya Mashariki ya Kati la kupendekeza mwongozo wa kumaliza vita hivyo ambavyo sasa vinaathiri uchumi wao.