Kimataifa

Israel yalegeza masharti baada ya kushutumiwa na Kanisa Katoliki

Na MASHIRIKA March 31st, 2026 Kusoma ni dakika: 2

JERUSALEM, Israel

ISRAEL imeondoa marufuku iliyoweka Jumapili iliyozuia viongozi wakuu wa Kanisa Katoliki kuingia katika Kanisa la Church of the Holy Sepulchre kwa Misa ya Mitende kutokana na malalamishi kutoka mataifa kadhaa ulimwenguni.

Maafisa wa utawala nchini Israel walitaja hali tete ya usalama na uwezekano wa Iran kutekeleza mashambulio ya makombora kujibu mashambulio dhidi yake yanayotekelezwa na wanajeshi wa Israel.

Hata hivyo, watawala sasa wamekubali kuwa “vikao vichache vya maombi vinaweza kufanywa” katika Wiki Takatifu kuelekea Sikukuu ya Pasaka.

Mnamo Jumapili polisi wa Israel walimzuia Kadinali Pierbattista Pizzaball, kiongozi wa Kanisa Katoliki jijini Jerusalem, kuingia katika Kanisa la Church of the Holy Sepulchre kuongoza misa ya Jumapili ya Mitende.

Msaidizi wa Kadinali huyo, Francesco Lelpo pia alizuiliwa kuingia katika kanisa hilo.

“Kwa hivyo, kwa mara ya kwanza ndani ya karne kadhaa, Wakuu wa Kanisa walizuiwa kusherehekea Ibada ya Jumapili ya Mitende katika Kanisa la Church of the Holy Sepulchre,” Kanisa Katoliki likasema kwenye taarifa Jumapili.

“Kisa hiki kinatoa mfano mbaya na ni dharau kwa mabilioni ya watu kote ulimwenguni, ambao katika wiki hii, wanatazama Jerusalem,” taarifa hiyo ikaongeza.

Maafisa wa polisi walisema kuwa maeneo yote takatifu jijini Jerusalem yalifungwa kutokana na sababu za kuisalama wakati huu ambapo Amerika na Israel kwa upande mmoja, zinashambulia Iran.

Wakati wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhan, uliojiri pia baadhi ya vita hivyo kuanza, Msikiti wa Al-Aqsa pia ulifungwa na waumini hawa kuruhusu kuingia humo.

Hata hivyo, kuzimwa kwa viongozi wakuu wa Kanisa Katoliki kuendesha Ibada ya Jumapili ya Matawi kulilaaniwa vikali na mabalozi wa Amerika, Italia, Ufaransa na Umoja wa Ulaya (EU) wakisema hatua hiyo ni ukiukaji wa uhuru wa kuabudu.

“Kwa kuwa makanisa na misikiti jijini Jerusalem yamezingatia kanuni inayopiga marufuku mkusanyiko wa zaidi ya watu 50, viongozi wawili wakuu wa Kanisa Katoliki hawakufaa kuzuiwa kuingia katika Kanisa la Church of the Holy Sepulchre.

Serikali haingefaa kuwanyika uhuru wao wa kuabudu,” akasema balozi wa Amerika nchini Israel Mike Huckabee.