Kundi la RSF Sudan lashutumiwa kurusha droni na kuua watoto 33 shule ya chekechea
KORDOFAN, SUDAN
WATU wasiopungua 50, wakiwemo watoto 33 waliuawa wakati shambulizi la droni katika eneo la Kordofan Kusini, Kalogi, linasemekana kulenga shule ya chekechea.
Kundi la wapiganaji kwa jina Rapid Support Forces (RSF), linalopigana na jeshi la nchi hiyo, lilishutumiwa kwa shambulio hilo la Alhamisi, na mtandao wa madaktari Sudan na jeshi.
RSF haikujibu mara moja kuhusu shambulizi hilo, na badala yake ikashutumu jeshi kwa kushambulia soko Ijumaa kwenye shambulizi la droni eneo la Darfur, kwenye bohari ya mafuta katika mpaka wa Adre na Chad.
Sudan imegubikwa na vita tangu Aprili 2023 wakati mvutano wa mamlaka ulizuka baina ya RSF na jeshi, vikosi vilivyokuwa marafiki.
Ripoti hizi hazikuweza kuthibitishwa kwa njia huru.
Kulingana na wizara ya masuala ya kigeni inayoegemea jeshi, shule hiyo ya chekechea ililengwa mara mbili kwa makombora yaliyovurumishwa na droni.
Raia na madaktari waliokimbia katika shule iliyolengwa walishambuliwa vilevile, ilisema.
Akijibu ripoti kuhusu shambulizi la Kalogi, msemaji wa shirika la Umoja wa Mataifa kuhusu watoto, Unicef, alisema: “Kuwaua watoto katika shule yao ni ukiukaji wa kutisha wa haki za watoto.”
“Watoto hawafai kamwe kulipia gharama ya machafuko,” alisema Sheldon Yett.
Shirika hilo, alisema, lilihimiza “pande zote kukomesha mara moja mashambulizi haya na kuruhusu msaada wa kibinadamu kuwafikia wanaouhitaji zaidi kwa njia salama bila vikwazo.”
RSF ilishutumu jeshi kwa kushambulia kivukio cha Adre kwa sababu kilitumiwa “kusambazia msaada na bidhaa za kibiashara.”
Kulingana na kundi la watafiti wanaofuatilia ghasia hizo kwa jina Sudan War Monitor, shambulizi hilo lilisababisha raia kujeruhiwa na uharibifu mkubwa kwa soko.
Jeshi halikuzungumza papo hapo kuhusu ripoti kutoka Darfur.
Likiwa limesakamwa kati ya jiji kuu la Sudan, Khartoum na Darfur, eneo hilo linalojumuisha Kordofan Kaskazini, Kordofan Kusini na Kordofan Magharibi limekuwa mstari wa mbele kwenye mapigano hayo.
Vita vya Kordofans – yenye idadi ya watu wapatao milioni nane, vimeshika kasi huku jeshi likisukuma kuelekea Darfur.
Kwingineko, washambulizi waliojihami kwa bunduki waliwaua watu 12 akiwemo mtoto mvulana wa miaka mitatu katika kisa cha ufyatuliaji risasi kwenye baa karibu na jiji la Pretoria, kulingana na polisi.
Msemaji wa Huduma ya Polisi Afrika Kusini (SAPS), Athlenda Mathe, alithibitisha shambulizi hilo la Jumamosi, kwamba jumla ya watu 25 walipigwa risasi ndani ya baa mjini Saulsville kilomita 18 kutoka Pretoria, akisema 14 walipelekwa hospitalini.
Polisi walisema watoto watatu ni miongoni mwa waliokufa kwenye ufyatuaji huo, wakijumuisha wavulana wawili wenye umri wa miaka mitatu na miaka 12 mtawalia na msichana mwenye umri wa miaka 16.
Shambulizi hilo lilifanyika katika kile Mathe alitaja kuwa “kituo haramu cha kuuzia pombe” – baa- ndani ya chumba cha malazi mwendo wa saa kumi unusu alfajiri ambapo watu watatu waliwafyatulia risasi kiholela kundi la wanaume waliokuwa wakibugia pombe.
Polisi hawakuarifiwa hadi mwendo wa saa kumi na mbili asubuhi.
Walisema msako umeanzishwa na kwamba kiini cha shambulizi hilo bado hakijajulikana.
Afrika Kusini, taifa ambalo limeendelea zaidi kiviwanda barani, inaandamwa na uhalifu na ufisadi uliokithiri unaoendeshwa na mitandao iliyopangwa vilivyo.