Makataa ya Iran kufungua Hormuz kuisha leo Trump akiwahakikishia ‘jehanamu’
WASHINGTON/DUBAI
AMERIKA na Iran zimepokea rasimu ya mpango wa kusitisha vita, lakini Iran imekataa kufungua Mkondo wa Hormuz baada ya Rais Donald Trump kutishia kuitumbukiza “jehanamu” isipofanya hivyo kufikia leo (Jumanne).
Mpango huo wa amani unahusu njia mbili za usitishaji wa vita ukifuatwa na makubaliano mapana yanayotarajiwa kukamilishwa kwa muda wa siku 15 hadi 29, duru zinazofahamu mapendekezo hayo zilisema jana.
Mkuu wa Jeshi la Paksitan, Asim Munir, amekuwa akiwasiliana “usiku kucha” na Makamu wa Rais wa Amerika JD Vance, balozi maalum Steve Witkoff na Waziri wa Kigeni wa Iran Abbas Araghchi, duru zilisema.
Hata hivyo, Iran ilishikilia kuwa haitafungua Mkondo wa Hormuz mpaka vita visitishwe kwa muda, afisa wa cheo cha juu nchini Iran, aliambia Reuters jana akiongeza kuwa Iran haitakubali makataa inapoangalia upya pendekezo hilo.
Amerika haionekani kuwa tayari kusitisha kabisa vita vinavyoendelea, afisa huyo alisema.
Jana, shirika la habari la Axios lilisema Amerika, Iran na wapatanishi kutoka ukanda wa Mashariki ya Kati walikuwa wakijadili masharti ya muafaka wa kusitishwa kwa vita kwa siku 45.
Lilisema muafaka huo unaweza kuchangia kukomeshwa kabisa kwa vita, likirejelea duru za Amerika, Israeli na za kikanda zenye ufahamu kuhusu mazungumzo hayo.
Reuters haikuweza kuthibitisha mara moja ripoti hiyo. Ikulu na Wizara ya Kigeni ya Amerika hazikujibu Reuters ilipozifikia kusaka kauli zao kuhusu suala hilo.
Mapendekezo
Wapatanishi walikuwa wakipendekeza awamu mbili ya muafaka, kulingana na ripoti hiyo.
Awamu ya kwanza ingekuwa usitishaji wa vita kwa siku 45; awamu ya pili ingekuwa makubaliano ya kuhusu kusitishwa kabisa kwa vita.
Anwar Gargash, mshauri wa Rais wa Umoja wa Milki za Kiarabu (UAE) alisema makubaliano yoyote sharti yatoe hakikisho la kufunguliwa kwa Mkondo wa Hormuz.
Alionya kuwa makubaliano yanayofeli kudumaza mipango ya nyuklia ya Iran pamoja na makombora na droni zake yatatoa nafasi kwa “misukosuko hatari eneo la Mashariki ya Kati.”
Hatua ya Iran kutekeleza mashambulio katika viwanda vya kawi ya petroli na meli zenye uhusiano na Israel katika nchi za Kuwait, Bahrain na UAE ni kielelezo cha uwezo wa nchi hiyo kupigana.
Hii ni licha ya madai ya kila mara ya Trump kwamba Amerika ilidai kufaulu kulemaza uwezo wa Iran kufanya mashambulio ya makombora na droni.
Mnamo Jumapili Trump alitishia hatua kali dhidi ya Iran ikiwa haitafikia makubaliano na ifungue Mkondo wa Hormuz kufikia mwisho wa muda wa makataa leo (Jumanne) huku akivisifu vikosi vya operesheni maalum kwa kumwokoa mwanajeshi wa angani aliyekwama nchini Iran.
Katika taarifa yake, iliyosheheni matusi, kupitia mtandao wake wa Truth Social, Trump alitishia kushambulia viwanda vya kawi na miundomsingi ya uchukuzi Iran, hatua ambayo wakosoaji wanasema itachukuliwa kama uhalifu wa kivita.
“Jumanne (leo) itakuwa Siku ya Kituo cha Kawi, na Siku ya Daraja, kwa wakati mmoja, nchini Iran,” akasema.
“Hakuwa na kingine sawa na hicho!!! Fungueni Mkondo enyi washenzi, la sivyo mtaishi Jehanamu. HEBU TIZAMA! Allah asifiwe. Rais DONALD TRUMP”.
Na katika mseto wa jumbe zilizowashangaza wafuasi, maadui sawa na masoko ya kifedha, Trump aliambia shirika la habari la Fox News Jumapili kwamba Iran inashiriki mazungumzo na makubaliano yanaweza kupatikana kufikia Jumatatu (jana).