Kimataifa

MAPIGANO: Israel sasa yalenga kumuua Ayatollah Khamenei kulemeza Iran

Na REUTERS June 18th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

TEHRAN, IRAN

KIONGOZI wa Kidini Iran Ayatollah Ali Khamenei sasa ndiye analengwa na Israel huku vita vikiendelea kwa siku ya sita leo kila upande ukirusha makombora.

Ayatollah ambaye ana usemi kuhusu masuala yote ya uongozi wa Iran amekuwa na msimamo mkali huku akipinga vikali matakwa ya Amerika kwenye mazungumzo ya kutaka Iran ikome kukuza kiwanda chake cha nuklia na kutengeneza silaha hatari.

Tangu vita vianze kati ya mataifa hayo mawili wandani wake wamekufa kwenye mashambulizi au uvamizi uliotekelezwa na Israel.

Wale ambao wameuawa ni makamanda wakuu wa kijeshi akiwemo kamanda mkuu Hossein Salami, kamanda mkuu wa jeshi la hewa Amir Ali Hajizadeh ambaye pia alikuwa akisimamia mpango wa kutengeneza bomu la atomiki kisha mkuu wa idara ya ujasusi Mohammad Kazemi.

Hawa waliouawa walikuwa washauri kati ya 15-20 wa Ayatollah ambao pia hujumuisha viongozi wengine wa kidini, wanasiasa na makamanda wa idara mbalimbali ya kijeshi.

Khamenei alikuwa mfungwa kabla ya mageuzi ya 1979 na alilemazwa kupitia mlipuko wa bomu kabla kuwa kiongozi wa dini mnamo 1989.

Anaonekana kumakinikia kudumisha mtindo wa uongozi wa Iran ili usiingiliwe na mataifa ya Magharibi hasa Amerika. Msimamo wake mgumu umesababisha awe adui mkubwa wa Israel.

Chini ya mfumo wa uongozi wa serikali ya Iran, Ayatollah ndiye anatoa amri kwa jeshi, ana mamlaka ya kutangaza vita na pia ana mamlaka ya kuwateua na kuwafuta kazi makamanda wa jeshi pamoja na majaji.

Japo ana washauri, yeye ndio hutoa uamuzi wa mwisho kuhusu masuala ya kitaifa.

Waziri wa Ulinzi Israel Katz ameonya kuwa Israel itahakikisha Ayatollah anamalizwa jinsi Saddam Hussein alivyouawa katika vita kati ya Iraq na Amerika mnamo 2003.

Mwanzo Amerika ilipindua serikali ya Iraq kisha Saddam akatorekea shimo kwenye janga na alipopatikana, alinyongwa

“Namwonya dikteta wa Iran dhidi ya kuendelea kutekeleza uhalifu na kurusha mabomu yanayowaua raia wa Israel. Akumbuke kuwa dikteta Saddam kutoka taifa jirani la Iraq aliuawa na alikuwa na msimamo mkali dhidi ya Israel,” akasema Katz.

Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu mwenyewe amenukuliwa akisema ni kupitia kumaliza utawala wa Ayatollah kwa kumuua, kutachangia amani ya kudumu na kukomesha tabia ya Iran ya kuendeleza udikteta ukanda wa Mashariki ya Kati.

Mwanawe Ayatollah, Mojtaba naye anaonekana kuwa katika nafasi nzuri ya kumrithi babake huku akihusishwa sana kwenye masuala ya uongozi.

Hasa Mojtaba amekuwa na uhusiano wa karibu na makamanda wa jeshi pamoja na idara zote za kiusalama na hata hupokezwa habari za kijasusi.