Mashujaa wa ukombozi Zimbabwe wakataa Mnangagwa kujiongezea muhula
HARARE, ZIMBABWE
WAPIGANAJI walioshiriki vita vya ukombozi wa Zimbabwe waliwasilisha kesi Mahakamani Jumanne kupinga marekebisho ya katiba ambayo yataongeza muhula wa kuhudumu kwa rais kutoka miaka mitano hadi saba.
Marekebisho haya yakikumbatiwa, basi Rais Emmerson Mnangagwa atasalia madarakani hadi 2030.
Mnangagwa, 83, anastahili kumaliza muhula wake wa pili mnamo 2028. Atakuwa amehudumu kwa miaka 10 kwa sababu kila muhula unasheheni miaka mitano.
Isitoshe, kumekuwa na uhasama mkali wa nani anastahili kurithi nafasi yake ndani ya chama tawala cha ZANU-PF. Rais huyo aliingia mamlakani baada ya mapinduzi ya kijeshi yaliyofanyika mnamo 2017 na aliyekuwa Rais Robert Mugabe (sasa marehemu) akaondolewa madarakani.
Rais Mugabe alihudumu kwa miaka 37 na wakati wa utawala wake alikuwa akiungwa sana na wazee ambao walipigania ukombozi dhidi ya Mbeberu na kumsaidia kuhakikisha Zimbabwe inapata uhuru 1980.
Wazee hao sita walioshiriki vita vya uhuru wamependekeza mabadiliko ambapo rais sasa atakuwa akichaguliwa na wabunge badala ya wananchi moja kwa moja jinsi ambavyo imekuwa ikifanyika.
“Mswada huo wa marekebisho ya katiba unalenga tu kuongeza muhula wa kutawala wa rais wa sasa,” ikasema stakabadhi za kesi kortini.
“Kinachosikitisha ni kwamba, hawataki kura ya maamuzi iandaliwe na badala yake wanataka mabadiliko haya yapitishwe kupitia bunge. Huu ni ukiukaji mkubwa wa katiba,” ikaongeza stakabadhi hiyo.
Hata hivyo, Msemaji wa Serikali Nick Mangwana alisema wazee hao wana haki ya kuenda kortini lakini hawatafaulu.
“Walioenda kortini ni wazee sita kati ya maelfu ya waliopigania uhuru wa Zimbabwe. Wana haki ya kuenda mahakamani na kuwakilishwa,” akasema.
Wakili wa wazee hao Lovemore Madhuku alisema marekebisho hayo kupigiwa kura bungeni ni njama ya Zanu-PF kutumia idadi yake kuyapitisha bila kupitia kura ya maamuzi.
“Iwapo mahakama itakubali, wazee hao watasaka amri ya kufuta mswada huo kabisa,” akaongeza.
Tayari Baraza la Mawaziri la Zimbabwe limetangaza kuwa linaunga mkono mswada huo.
Waziri wa Katiba Ziyambi Ziyambi wiki hii alisema mswada huo utapelekwa kwa Spika wa Bunge kisha uchapishwe kwenye gazeti rasmi la serikali kabla ya wabunge kuanza kuutathmini.
Jameson Timba, ambaye ni kati ya viongozi wa upinzani unaoonekana kudhoofika kiushawishi kupitia taarifa alisema hatua ya Baraza la Mawaziri kuidhinisha marekebisho hayo ya katiba yatakosesha taifa hilo udhabiti wake.