Kimataifa

Mazungumzo kuhusu Hormuz yasambaratika baada ya Amerika na Iran kukosa kuafikiana

Na REUTERS April 12th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

ISLAMABAD, PAKISTAN: 

AMERIKA na Iran zilikosa kuafikiana kumaliza vita vyao licha ya misururu ya mazungumzo yaliyokamilishwa Jumapili asubuhi katika jiji kuu la Islamabad, na kuhatarisha juhudi dhaifu za kusitisha mapigano.

Kila upande ulilaumu mwingine kwa kusambaratisha majadiliano ya saa 21 ya kumaliza vita ambavyo vimewaua maelfu, kutikisa uchumi wa dunia na kusababisha bei za mafuta kupanda tangu vilipoanza zaidi ya wiki sita zilizopita.

“Habari mbaya ni kuwa hatujapata maafikiano, na nafikiri hizo ni habari mbaya kwa Iran sawia na zilivyo habari mbaya kwa Amerika,” alisema Makamu wa Rais wa Amerika JD Vance, aliye kiongozi wa wajumbe wa Amerika katika mazungumzo hayo.

“Hivyo basi tunarejea Amerika pasipo kufanikisha mkataba. Tumeeleza wazi vipimo vyetu ni vipi.”

Spika wa Bunge la Iran Mohammad Baqer Qalibaf, aliyeongoza wajumbe wa taifa lake pamoja na Waziri wa Masuala ya Kigeni, Abbas Araqchi, walilaumu Amerika kwa kukosa kushinda imani ya Iran licha ya timu yake kutoa “mikakati inayotazama mbele.”

“Amerika imeelewa mawazo na kanuni za Iran na wakati umewadia kwao kuamua iwapo wanaweza kuvutia imani yetu au la,” alisema Qalibaf kwenye mtandao wa kijamii wa X.

Wajumbe wa Amerika na Iran wote wameondoka Islamabad kurejea nyumbani, duru za Pakistani zilieleza Reuters.

Mazungumzo hayo, baada ya hatua ya kusitisha mashambulizi mapema wiki jana, ni mkutano wa kwanza wa moja kwa moja kati ya Amerika na Iran kwa zaidi ya mwongo mmoja na mazungumzo ya ngazi za juu zaidi tangu Mageuzi ya Kiislamu 1979.

Vance alisema Iran ilichagua kutokubali matakwa ya Amerika, ikiwemo kukoma kuunda silaha za kinuklia.

“Tunataka ahadi thabiti kuwa hawatasaka silaha ya nuklia na hawatasaka nyenzo zitakazowawezesha kufanikisha upesi silaha ya nuklia,” alisema.

“Hiyo ndiyo shabaha kuu ya rais wa Amerika, na hilo ndilo tumejaribu kufanikisha kupitia majadiliano haya.”

Kituo kisicho rasmi cha habari Iran kilisema matakwa “tele kupindukia” ya Amerika yalizuia kufanikisha mkataba.

Vituo vingine vya habari vilisema kulikuwa na maafikiano kuhusu masuala kadhaa lakini Mkondo wa Hormuz na mpango wa nuklia wa Iran yalikuwa masuala nyeti yaliyozua utata.

Waziri wa Masuala ya Kigeni Pakistan Ishaq Dar alisema ni “muhimu” sana kuhifadhi mkataba wa wiki mbli wa kusitisha uhasama ulioafikiwa Jumanne huku pande husika zikijaribu kutuliza vita vilivyoanza Februari 28 kwa mashambulizi ya angani yaliyotekelezwa na Amerika na Israeli dhidi ya Iran.

Waziri wa Usalama Israeli, Zeev Elkin alieleza Redio ya Jeshi kwamba mazungumzo zaidi ni hiari lakini akasema: “Raia wa Iran wanacheza na moto.”

Katika hotuba fupi kwa vyombo vya habari, Vance hakutaja kufunguliwa upya kwa Mkondo wa Hormuz, kituo muhimu cha kusafirisha takriban asilimia 20 ya bidhaa za nishati duniani ambacho Iran imefunga imefunga tangu vita vilipoanza.

Vance alisema alizungumza na Rais Donald Trump mara kadhaa wakati wa mazungumzo hayo.

Hata mazungumzo yalipokuwa yakiendelea, Trump alisema Jumamosi mkataba si lazima uafikiwe.

“Tunajadiliana. Iwe tutaafikiana kuhusu mkataba au la haina tofauti kwangu, kwa sababu tumeshinda,” alieleza wanahabari.