Kimataifa

Mojtaba bado mafichoni duru zikisema huenda alijeruhiwa

March 12th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

TEHRAN, IRAN

WANAJESHI wa Iran walilazimisha uteuzi wa Mojtaba Khamenei kuwa Kiongozi mpya wa kidini wakisisitiza ndiye anaweza kuendeleza uongozi wenye msimamo mkali.

Duru kutoka Iran ziliarifu kuwa wanajeshi hao walikiuka mtazamo wa baadhi ya wanasiasa wa ngazi ya juu na viongozi wa kidini ambao walikuwa wamepinga uteuzi wa Mojtaba kama Ayatollah mpya.

Kufikia Jumanne, saa 48 baada ya Mojtaba kuteuliwa, waliopinga uteuzi wake bado hawakuwa wametoa taarifa.

Isitoshe Mojtaba mwenyewe hajajitokeza na kuzungumza hadharani tangu ateuliwe mrithi wa babake marehemu Ayatollah Khamenei ambaye aliuawa na wanajeshi wa Amerika-Israeli.

Mojtaba amekuwa mhimili mkubwa wa uongozi wa babake lakini duru hizo zinaarifu huenda hajajitokeza hadharani kwa sababu alijeruhiwa na wanajeshi wa Amerika-Israel i wakati baadhi ya wanafamilia wake waliangamia.

Mtangazaji wa runinga alionekana kuthibitisha kuwa Mojtaba alijeruhiwa baada ya kumrejelea kama ‘janbaz’ (mpiganaji aliyejeruhiwa) wakati wa vita ndani ya Mwezi Mtukufu wa Ramadhan.

Hadi leo bado hajaonekana hadharani au haijulikani jinsi hali yake ya kiafya ilivyo.

Baada ya babake kuuawa mnamo Febrauri 28 Kamati ya Wataalamu yenye wanachama 88 ilitangaza Jumapili kuwa aliteuuliwa Kiongozi wa Kidini wa Iran.

Mnamo Jumamosi, Rais Masoud Pezeshkian alionekana kuwachemsha wanajeshi hao baada ya kuomba msamaha kwa mataifa ya Ukanda wa Gulf.

Rais Pezeshkian alikuwa amesema kuwa Iran haitashambulia tena nchi hizo ambazo zina kambi za mafunzo kwa wanajeshi wa Amerika.

Inadaiwa wanajeshi walikerwa na msamaha huo na kumwonya rais huyo.

Marehemu Ayatollah Khamenei alikuwa akisawazisha uongozi wa urais na maoni ya wanajeshi kabla ya kutoa mwelekeo.

“Uaminifu kwa Mojtaba utakuwa kwa wanajeshi ambao walimpa mamlaka kwa hivyo huenda hatakuwa na nguvu za kuamua mambo kivyake jinsi alivyokuwa babake,” akasema Alex Vantaka, mwanahabari Ukanda wa Mashariki ya Kati.

Kuna hofu kuwa Iran sasa inachukua mkondo wa utawala wa kijeshi ambapo wao ndio watakuwa wakiamua masuala muhimu licha ya uwepo wa Mojtaba.

Aidha imebainika kuwa kutokana na vita kuchacha, kamati ya wataalamu ilikuwa na msukumo wa kumteua mrithi wa Ayatollah Khamenei ili kusiwe na pengo na kukosekane mwelekeo wa kivita.

Mojtaba pia inasemekana wakati wa uongozi wa babake, alikuwa na uhusiano wa karibu na makamanda wa kijeshi ambao wamechukua nafasi za wale waliouawa vitani.

Haya yanajiri siku moja tu baada ya Rais wa Amerika Donald Trump kusema Amerika itamlenga Mojtaba Khamenei.

Trump pia alisisitiza kuwa hawezi kumkubali Mojtaba kwa sababu ataendeleza tu msimamo mgumu kama tu ya Ayatollah Khamenei.

Alisema Iran ‘inapoteza wakati wake’ kwa Mojtaba huku akisema kuwa mwana huyo wa pili wa kiume wa marehemu Ayatollah Khamenei ni ‘mwepesi’ kwake.

“Kiongozi mpya Iran hatahudumu kwa kipindi kirefu iwapo atateuliwa bila idhini yetu, hatahudumu,” akasema Trump.

Saa chache baada ya tamko la Trump, Iran nayo ilitangaza Mojtaba kama mrithi wa babake.

“Tunataka kuhakikisha kwamba haturudi nyuma kila baada ya miaka 10 mkiwa hamna rais kama mimi,” akaongeza.