Kimataifa

Ndege iliyokuwa ikielekea London yaanguka na kuua zaidi ya abiria 200

Na REUTERS June 12th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

AHMEDABAD, India

WAU zaidi ya 200 wamefariki baada ya ndege ya Air India iliyokuwa ikielekea London na abiria 242 kuanguka dakika chache baada ya kupaa kutoka jiji la Ahmedabad magharibi mwa nchi hiyo.

Polisi walisema mtu mmoja angalau ameokoka, na aliambia vyombo vya habari vya India kwamba alisikia mlipuko mkubwa muda mfupi baada ya kupaa.

Ndege hiyo ilianguka katika eneo la makazi, na kugonga bweni la chuo cha udaktari karibu na uwanja wa ndege wakati wa chakula cha mchana. Ilikuwa ikielekea Uwanja wa Ndege wa Gatwick, kusini mwa jiji kuu la Uingereza.

Kamanda wa polisi wa jiji, G.S. Malik, aliambia Reuters kwamba miili 204 ilipatikana katika eneo la ajali. Afisa mwingine wa cheo cha juu wa polisi, Vidhi Chaudhary, alisema walimpata mtu mmoja aliyenusurika, aliyekuwa ameketi katika kiti cha 11A, na kuongeza kuwa huenda kuna manusura zaidi hospitalini.

“Sekunde 30 baada ya kupaa, kulikuwa na kelele kubwa kisha ndege ikaanguka,” alisema Ramesh Viswashkumar, mwenye umri wa miaka 40, aliyezungumza na Hindustan Times, ambaye pia alionyesha tiketi ya kiti cha 11A kwa jina lake.

“Yote yalitokea kwa haraka sana,” aliambia gazeti hilo akiwa kitandani hospitalini.

“Niliposimama, miili ilikuwa kila mahali karibu nami. Niliogopa. Nilisimama na kukimbia. Vipande vya ndege vilikuwa vimezagaa kila mahali,” alisema.

“Mtu alinichukua na kuniweka kwenye ambulensi na kunipeleka hospitalini.”

Aliongeza kuwa kaka yake, Ajay, alikuwa ameketi sehemu nyingine ndani ya ndege hiyo.

“Alikuwa akisafiri pamoja nami na siwezi kumpata tena. Tafadhali nisaidieni kumpata,” alisema.

Kamanda Malik alisema miili iliyopatikana huenda ikajumuisha abiria na watu waliokuwa ardhini. Waziri wa serikali kuu, C.R. Patil, alisema miongoni mwa waliokufa ni Vijay Rupani, aliyekuwa waziri wa jimbo la Gujarat, ambalo mji wa Ahmedabad ni mji mkuu wake.

“Kuna uwezekano wa kuwa na manusura zaidi miongoni mwa waliolazwa hospitalini,” alisema afisa Chaudhary.

“Pia kuna uwezekano idadi ya vifo ikaongezeka. Watu zaidi ya 50 waliojeruhiwa wako hospitalini kwa sasa.”

Ndugu wa marehemu waliombwa kutoa sampuli za DNA ili kusaidia kuwatambua waliokufa, kwa mujibu wa katibu wa afya wa jimbo, Dhananjay Dwivedi.