Kimataifa

Papa Leo XIV amtimua askofu kwa wizi

Na MASHIRIKA March 11th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

VATICAN CITY

PAPA Leo amekubali kujiuzulu kwa Askofu wa Kanisa Katoliki wa San Diego ambaye alinyakwa kwa wizi wa Sh32 milioni kutoka kwa waumini wake.

Vatican ilithibitisha kuwa askofu huyo, Emanuel Hana Shaleta, ameondolewa kwenye wadhifa wake.

Amekuwa akiongoza waumini kutoka kwenye eneo la Chaldean, California, Amerika tangu 2017.

Kulingana na vyombo vya habari San Diego, Shaleta alikanusha mashtaka 16 ya ufujaji na ulanguzi wa fedha wakati wa kusikizwa kwa kesi hiyo.

Naibu Mkuu wa Sheria wa San Diego Joel Madero alisema wizi huo ulitokea mnamo 2024 na uliripotiwa na muumini wa kanisa hilo.

Muumini huyo alipiga ripoti baada ya kubaini kuwa kulikuwa na pesa ambazo zilipotea.

Hana Shaleta alikamatwa mnamo Machi 5 katika uwanja wa kimataifa wa ndege wa San Diego akijaribu kutoroka Amerika.

Hata hivyo, wakili wake alisema alikuwa akielekea safari iliyokuwa imepangwa hapo awali Ujerumani.

Wakatoliki wa Chaldean wanatambua mamlaka ya Papa lakini wao huabudu kwa msingi wa dini ya Kikristo wenye asili ya Ugiriki.

Takwimu za Vatican zinaonyesha kuwa kuna zaidi ya Wakatoliki 71,000 wa Chaldean San Diego.