Raha Malaysia meli zao zikifaulu kupita Mkondo wa Hormuz
KUALA LUMPUR
WAZIRI Mkuu wa Malaysia Anwar Ibrahim mnamo Alhamisi alisema kuwa alizungumza na viongozi wa Iran, Misri, Uturuki na mataifa mengine ya kikanda na mazungumzo hayo yakasababisha meli zao za mafuta ziruhusiwe kupita kwenye njia ya Strait of Hormuz.
Akionekana kuwa na furaha tele akihutubu kwenye runinga ya serikali, Anwar alishukuru sana uongozi wa Iran kwa kuruhusu meli hizo kupita eneo hilo.
“Sasa tumeanza kuachilia meli hizo za mafuta ziendelee na safari pamoja na wafanyakazi ambao wapo,” akasema.
Anwar alifichua kuwa aliongea na Iran pamoja na mataifa mengine ya Ukanda wa Mashariki ya Kati ili kuhakikisha kuna amani.
“Amani si rahisi kwa sababu Iran inahisi inahadaiwa bila mwongozo maalum wa kuhakikisha amani. Hakuna hakikisho kuwa kutakuwa na amani iwapo Iran itarejea kwenye mazungumzo,” akasema Anwar.
Kiongozi huyo sasa amewaondolea raia wa taifa lake hofu kuwa kutakuwa na uhaba wa mafuta akisisitiza kuwa serikali yake pia itaendelea kudumisha ruzuku inayotoa kudhibiti bei ya mafuta.
“Tulikuwa tumeanza kuathirika kwa sababu ya meli kuzimwa kupitia Mkondo wa Hormuz kwa kuwa vita bado vinaendelea. Sasa hatuna wasiwasi wowote kuwa hali itakuwa sawa,” akaongeza