Rais Kiir afuta waziri wa fedha aliyeajiri Novemba
JUBA, SUDAN KUSINI
RAIS wa Sudan Kusini, Salva Kiir, mnamo Jumatatu alimtimua Waziri wa Fedha Bak Barnaba Chol kwenye mabadiliko katika Baraza la Mawaziri yaliyopeperushwa kwenye runinga ya serikali.
Chol aliteuliwa kama waziri wa fedha mnamo Novemba mwaka jana baada ya Kiir kumfuta Athian Diing Athian miezi miwili baada ya kumteua.
Kiir alimteua Salvatore Garang, mwanauchumi ambaye alipokea mafunzo kutoka Chuo Kikuu cha Khartoum kama waziri mpya wa fedha.
Garang awali alihudumu kama Waziri wa Fedha kutoka 2018 hadi 2020, kipindi ambacho Sudan ilishuhudia mabadiliko makubwa kiuchumi.
Katika kipindi hicho, vyombo vya habari hata hivyo viliripoti kuwa Garang alikabiliwa na madai ya ufisadi ikiwemo kutenga Sh12.9 milioni kugharamia mazishi ya mwanawe wa kiume.
Kama kawaida hakuna sababu ambazo zilitolewa kwenye mabadiliko yaliyofanyika kwenye wizara hiyo ya fedha.
Pia amri aliyotoa ilimwondoa madarakani mkuu wa Mamlaka ya Ukusanyaji Ushuru Sudan Kusini. Kwa upande mwingine, alimfuta Monica Achol Abdel Aguek kama Balozi wa Afisi ya Rais kuhusiana na Masuala ya Ukanda wa Afrika Mashariki, wadhifa ambao ameushikilia tangu Novemba 2025.
Pia mkuu wa Mamlaka ya Ukusanyaji Ushuru William Anyuon Kuol na Naibu wake Moses Rou Ayii waliathirika.
Nafasi zao zilichukuliwa na Balozi Muon Deng Ajuet na Solomon Ariik Manyok mtawalia.
Wachanganuzi wa masuala ya kisiasa wanasema kuwa Kiir amekuwa akiyatekeleza mabadiliko ya mara kwa mara katika utawala wake na jeshi ili kuendelea kudhibiti serikali.
Amekuwa akipambana na mzozo wa kisiasa na mirengo mbalimbali na pia kuna siasa za urithi ambazo zimeanza kumlemea.
Mchanganuzi wa masuala ya sera Boboya James Edimond alisema kuwabadilishabadili sha mawaziri wa fedha kunaonyesha udhaifu wa kiuchumi na hautatatua changamoto za kifedha zinazoandama Sudan.
Alisema mabadiliko kwenye wizara ya fedha na mamlaka ya kukusanya ushuru huenda yanasukumwa na haja ya kupatikana kwa fedha zaidi kugharimia shughuli za serikali na kulipa mishahara.
“Serikali kwa sasa haina pesa. Na matukio haya yanaonyesha tu jinsi ambavyo ufisadi umekolea na mifumo ya uwajibikaji na usimamizi wa fedha kuvurugwa.
“Hawa watu ambao wanateuliwa na kutimuliwa hawana uwezo wa kubadilisha hali. Wao ni watu binafsi na si taasisi,” akasema Edimond.
Mnamo Novemba mwaka jana vuguvugu la wanawake lilitoa wito kwa Kiir amteue mwanamke kama waziri wa fedha likisema wanaume ambao wamehudumu katika wadhifa huo sio wachapakazi.
Tangu achukue madaraka, serikali ya Kiir imekuwa ikikumbwa na matatizo kadhaa.