Kimataifa

Rais Salva Kiir wa Sudan Kusini akilala akiamka, kazi ni kufuta

Na REUTERS April 9th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

JUBA, SUDAN KUSINI

RAIS wa Sudan Kusini Salva Kiir halali hakeshi huku akiendelea kukumbatia mtindo wa kuwafuta maafisa wa ngazi ya juu katika serikali yake bila kuonekana kuchoka.

Kiir mnamo Jumatano aliwatimua Spika wa Bunge la Kitaifa na Naibu Spika.

Kiranja wa Chama tawala cha SPLM Tulio Odongi Ayahu, alitangaza kuondolewa kwa Spika Jemma Nunu Kamba na Naibu Spika Permana Awerial Aluong kutoka nyadhifa zao kwenye Bunge la muda la kitaifa.

Hatua hiyo, inafuatia malalamishi ya wanachama wa SPLM ambao walimshutumu Kumba kwa kushiriki ufisadi.

Hasa walimhusisha na sakata ya matumizi mabaya ya fedha za Bunge na kutoa wito atimuliwe.

Kumba aliandikisha historia mnamo 2021 kama spika wa kwanza mwanamke kuhudumu katika Bunge la Kitaifa la Sudan.

Hata hivyo, bado hajajibu madai dhidi yake.

Kiir aliwateua Joseph Ngere Paciko na Abuk Paiti Ayiik kama spika na naibu mpya wa spika mtawalia.

Futafuta hizo zilitokea baada ya Kiir mnamo Februari kumfuta kazi aliyekuwa Waziri wa Fedha Bak Barnaba Chol ambaye alikuwa afisini kwa miezi mitatu pekee, akikosa kutoa sababu zozote za kuchukua hatua hiyo.

Wachanganuzi wa masuala ya kisiasa wanasema futafuta za Kiir katika jeshi na bunge zinalenga kuhakikisha anadhibiti utawala wake wakati ambapo siasa za urithi zimeshika kasi kutokana na afya yake kudorora.