Kimataifa

Seneta wa Amerika akataa ombi la msamaha la Muhoozi

Na ANTHONY KITIMO February 1st, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KIONGOZI mkuu wa bunge la Seneti Amerika ameonya kuwa Jenerali wa Uganda Muhoozi Kainerugaba, ambaye pia ni mwana wa Rais Yoweri Museveni, alivuka mpaka hatari unaoweza kuathiri vibaya uhusiano wa kidiplomasia kati ya nchi hizo mbili.

Mwenyekiti wa Kamati ya Masuala ya Kigeni ya Seneti ya Amerika Seneta Jim Risch wa chama cha Republican, alisema Jenerali Muhoozi hakufuata itifaki za kidiplomasia alipoomba Amerika msamaha kuhusu madai yake ya ukiukaji wa haki za binadamu ulioshuhudiwa wakati wa Uchaguzi Mkuu Uganda mwaka wa 2026.

“Kamanda @mkainerugaba amevuka mipaka na sasa Amerika inalazimika kutathmini upya ushirikiano wake wa kiusalama, ikiwemo kuweka vikwazo na ushirikiano wa kijeshi na Uganda. Mwana wa rais, na anayechukuliwa kama mrithi wake, hawezi kufuta tu ujumbe mitandaoni na kuomba msamaha juujuu. Amerika haitakubali kiwango hiki cha utovu wa nidhamu na uzembe wakati wanajeshi wa Amerika, maslahi ya Amerika na maisha ya raia wasio na hatia katika eneo hili yako hatarini,” Seneta Risch alisema kupitia ujumbe alioutuma katika mtandao wa kijamii wa X.

Tume ya Uchaguzi ilimtangaza Rais Yoweri Museveni mshindi wa uchaguzi wa Januari 15, na kumpa muhula wa saba, hivyo kurefusha utawala wake hadi zaidi ya miaka 40.

Seneta Risch alipuuza matokeo hayo akisema hayakuwa halali na yalilenga tu kuendeleza utawala wa Museveni.

Alitaja uchaguzi huo kama zoezi tupu lililoandaliwa kuhalalisha muhula wa saba wa rais na miongo minne ya utawala wake.

Seneta huyo alilinganisha uchaguzi wa Uganda na ule wa hivi karibuni wa Tanzania, lakini akasema hali ya Uganda inatia wasiwasi zaidi kutokana na uhusiano wa karibu wa kiusalama kati ya nchi hiyo na Amerika.

Muda mfupi baada ya kauli ya Seneta Risch, Jenerali Muhoozi alitangaza kuchukua mapumziko katika mitandao ya kijamii baada ya kuichangamkia kwa zaidi ya miaka 11.

“Baada ya takriban miaka 11 kwenye Twitter/X na baada ya kupata zaidi ya wafuasi milioni 1.2, ninakusudia kupunguza kushiriki kwangu hapa. Ninarudi kufunga na kuomba kwa ajili ya nchi yangu. Kwa msaada wa Mungu nalenga kubadilisha wasifu wangu,” alisema Jenerali Muhoozi kupitia X.

Jenerali Muhoozi alizua ghadhabu kimataifa kupitia mitandao ya kijamii baada ya uchaguzi huo, ikiwemo kutangaza kusitishwa kwa ushirikiano wote kati ya Jeshi la Ulinzi la Uganda (UPDF) na ubalozi wa Amerika mjini Kampala.

Pia alichapisha jumbe kadhaa ambazo baadaye alifuta, akidai miongoni mwa mambo mengine kuwa vikosi vya usalama viliwaua “magaidi” 22 wa upinzani na kupendekeza kuwa kiongozi wa upinzani Bobi Wine angefuata.

“Tumeua magaidi 22 wa NUP tangu wiki iliyopita. Ninaomba wa 23 awe Kabobi,” aliandika, akitumia jina la dhihaka kumrejelea kiongozi huyo wa upinzani.

Katika ujumbe mwingine, alimpa Bobi Wine saa 48 ajisalimishe kwa polisi, akionya kuwa asipofanya hivyo angechukuliwa kama “mhalifu au muasi”.

Jenerali Muhoozi pia aliapa kuondoa kabisa Chama cha National Unity Platform (NUP) katika siasa za Uganda, akidai kuwa alikuwa na mamlaka ya kiungu kufanya hivyo.

Baadaye aliomba msamaha na kusisitiza kuwa uhusiano wa pande mbili bado uko imara, akisema alipotoshwa alipodai kuwa Amerika ilimuunga mkono kiongozi wa upinzani, Bw Robert Kyagulanyi, ambaye amekuwa mafichoni tangu uchaguzi huo wa Januari 15.

“Ningependa kuwaomba radhi marafiki wetu wakubwa, Amerika, kwa jumbe zangu za awali ambazo sasa nimezifuta. Nilikuwa na taarifa zisizo sahihi,” Muhoozi aliandika.

“Nilizungumza na Balozi wa Amerika nchini mwetu, na kila kitu kiko sawa. Tutaendelea na ushirikiano wetu wa kijeshi kama kawaida.”