• Nairobi
  • Last Updated May 5th, 2024 6:07 PM
SIASA ZA SUDAN: Hali halisi ya utovu wa demokrasia

SIASA ZA SUDAN: Hali halisi ya utovu wa demokrasia

NA TAREK CHEIKH 

Uasi dhidi ya serikali unasambaa kote nchini Sudan. Kilichoko hatarini si hatima ya Rais Omar al-Bashir pekee, bali mfumo mzima wa utawala wa nchi.

Alipokamatwa mwanzoni mwa miaka ya 1970, akiwa njiani kuelekea gerezani mshairi maarufu wa Sudan Mahjoub Sharif aliandika sala iliyojaa shauku:

Lini litasafika,

Anga la Khartoum yetu pendwa,

Lini yataponyeka,

Majeraha ya taifa.

Miongo kadha baadaye, yaelekea kuwa swali lake linajibiwa. Asubuhi ya Desemba 25, mji mkuu wa Sudan uliamka kushuhudia kelele kubwa za uasi, zinazohusisha makundi kadhaa ya upinzani katika maandamano makubwa kabisa kuwahi kutokea tangu chama cha Rais aliyekuwa madarakani Omar al-Bashir’s cha Islamist Movement kilipoingia madarakani kwa kuipindua serikali iliyokuwepo mwaka 1989.

Mwito wa kuhamasishana ulitolewa na Muungano wa Wafanyakazi, ambao huvikutanisha vyama vikubwa vya wafanyakazi vya madaktari, wahandisi, wanasheria, na waandishi wa habari, na kuungwa mkono na raia pamoja na baadhi ya vyama vya siasa – muunganiko ambao haujawahi kutokea kwa miongo kadhaa.

Lengo lililotamkwa awali na Muungano wa Wafanyakazi, ulioko Khartoum, lilikuwa kuwasilisha serikalini msimamo wa vyama vya wafanyakazi kupinga sera ya uchumi.

Lakini mwamko wa kisiasa uliojitokeza ulipelekea kundi hilo liongeze ukubwa wa matakwa yake ikiwemo barua kwenda ikulu ikimtaka wazi raisi ajiuzulu.

Ikikabiliwa na harakati ya kushtusha inayoendelea katika miji mikubwa na midogo, serikali inaonekana kusitasita kati ya kufanya hila na kukubali mabadiliko, ama kurejea kwenye matumizi ya nguvu ambayo taifa hili limeyazoea kwa miongo zaidi ya mitatu iliyopita.

Mapinduzi

Tangu ipate uhuru kutoka kwa Waingereza mwaka 1956, Sudan imepitia mapinduzi kadhaa maarufu, mawili kati yao yakifanikiwa kuwaondoa madarakani watawala Madikteta: Kamanda Ibrahim Abboud mwaka 1964, kisha Jenerali Jaafar Nimeiry mwaka 1985. Lakini uasi wa sasa unaonekana tofauti na uasi mwingine uliowahi kutokea kwa kila namna.

Kama uasi uliotangulia ulijikita katika harakati za vyama vya wafanyakazi vilipokuwa na nguvu kubwa, na harakati za kisiasa zilizopangwa vema katika miji mikubwa ya Sudan, hususan ndani jiji kuu, uasi wa sasa ulijengeka katika miji iliyo kaskazini mbali na jiji kuu kama Atbara, ambao kihistoria ni eneo la tabaka la wafanyakazi na mahali ambapo chimbuko la harakati za muungano wa wafanyakazi wa Sudan lilizaliwa.

Kisha ulisambaa haraka, mawimbi yake yakipiga miji mingine jirani ya kaskazini kama Berber na Damer, kisha Danqala na Karima. Uasi ulielekea mashariki, huko Qadarif, Port Sudan na Kasla, kisha magharibi, huko Ubayyid, Rahad, na katika eneo mkabala na mto Nile mweupe.

Harakati hii maarufu imeleta pamoja makundi tofauti tofauti ya jamii. Tetemeko hili la kisiasa limewashtusha watawala wa dola, ambao wamekuwa wakipendelea kuweka nguvu zao ndani ya jiji kuu ili kuzuia mapinduzi ya kuangusha serikali.

Zaidi ya nguvu na uhai wa harakati hii, uwazi wa matakwa yake ya kisiasa umeitia hofu serikali. Licha ya kushamiri kwa malalamiko ya tatizo la njaa na umaskini, matakwa haya si ya kiuchumi tu.

Shirika la Maendeleo ya Umoja wa Mataifa (UNDP) imekadiria kuwa zaidi ya watu milioni ishirini nchini Sudan wanaishi chini ya mstari unaotenganisha watu masikini.

Ni Dhahiri kuwa kauli mbiu wanazopigia kelele waandamanaji katika miji yote ni za kisiasa. Maneno wanayotumia waandamanaji kupiga kelele mara kwa mara ni “uhuru, Amani na Haki” na “Mapinduzi ni Chaguo la Wananchi”, ikionyesha kina cha matamanio ya wengi, na nguvu ya wazo la mapinduzi.

Mabadiliko haya makubwa ya ghafla – bila maandalizi – yameifikisha harakati katika kiwango kisichokuwa kimetarajiwa: Licha ya umaskini na njaa, watu wameonyesha wazi matamanio yao ya kumalizana na utawala wa chama cha National Islamic Front chenye ukaribu na chama cha Muslim Brotherhood na kuanza zama mpya.

Ni wazi pia kuwa chama tawala cha Harakati za Kiisilamu kimeishiwa mvuke kabisa, kikiacha nyuma kikiacha urithi wa historia ya ukandamizaji: unayo husisha kuhusika kwa dola katika kila hatua kila nyanja, kutoka nyanja za kiuchumi hadi zile za kisiasa na kitamaduni, na, kama vile kitendawili, katika nyanja ya kidini, ukizingatia uharibifu unaoletwa na mchanganyiko dhalimu wa dini na rushwa.

Wakati wa mkutano na wahariri mahiri wa vyombo vya habari vya Sudan, Mkuu wa usalama wa Taifa Salah Guoch alisema aliamini harakati hii ilikuwa ni uasi wa kawaida usiohusika na vyama vya siasa.

Kwa kutovihusisha vyama vya siasa, Guoch alikuwa anasema kwamba aliamini harakati hii maarufu haikuwa na matumaini – hoja ambayo kwa haraka ilipingwa na hali halisi.

Alililaumu hasa kundi la Sudan Liberation Movement, ambalo ni kundi la kujitenga la Darfuri linaloongozwa na Abdul Wahid al-Nour.

Shutuma hizo zinasaliti mshituko wa serikali iliyokabiliwa na mapinduzi. Maeneo ambako ofisi za chama tawala cha National Congress zimevamiwa na kuharibiwa (Atbara, Damer, and Berber) zinahusisha katika jamii zake kiasi kidogo sana cha watu wa jamii ya Darfuri, na kwa hakika zinahusishwa — na dola, bila shaka — chimbuko la harakati za kiisilamu.

Maandamano

Maandamano haya maarufu yanaendelea; kila kitu kinaachiria kuwa wakazi wa mijini wamechukua hatamu ya kuyaongoza. Wananchi katika miji na majiji mbalimbali wamethubutu kukabiliana na tatanzo la hari ya hatari na marufuku ya kutoka majumbani.

Tukio lililo muhimu kabisa kufikia sasa bila shaka ni matukio ya  Decemba 25, ambapo kila ujirani ulichukuliwa na makundi ya waandamanaji.

Mbele ya kila wanaoandamana, walitembea wawakilishi wa vyama vya wafanyakazi wa sekta mbalimbali, pamoja na viongozi wa vyama vya siasa.

Maandamano haya ni ya kwanza kuwa na mvuto wa hali ya juu tokea mapinduzi ya serikali yaliyofanywa na al-Bashir’s mwaka 1989.

Licha ya dola kutumia nguvu kupita kiasi, na matumizi ya risasi za moto kutawanya waandamanaji, kutokana na dhamira yao thabiti ya kuwapinga wenye mamlaka, wananchi wametoa ujumbe wazi kuwa mapinduzi sasa yako njiani , tena yakiwa na nguvu na uhai zaidi.

Kati ya jiji kuu sasa panaonekana kama uwanja wa vita pakiwa pamejazwa askari wengi na magari ya kivita. Kwa kipindi hiki kinachoendelea, kazi ya muungano wa vyama vya wafanyakazi imekuwa na mafanikio makubwa, kama ilivyoandikwa katika tamko la Muungano wa Wafanyakazi. Imeizishutumu mamlaka kwamba:

“Kusambaza vyombo vya ulinzi na askari kwa maelfu, wakiwa na magari ya kivita, ambao wamepiga silaha za moto dhidi ya waandamanaji ili kuwazuia kukutana na wadau wa asasi za kiraia na vyama vya kisiasa, na kuzuia wingi wa raia wa Sudan wasije kuingia eneo la ikulu ili kutoa ujumbe unaomtaka rasi ajiuzulu.

Vyama vya wafanyakazi vimesherehekea mafanikio ya kuungana jambo ambalo limekuwa gumu kufanikiwa kwa miongo kadhaa: “Tumeelezea msimamo wetu thabiti, kuwa ni matakwa ya watu walioungana.” Ni mazingira yanayodhihirisha kujiamini – makundi yaliyokusanyika pamoja wanaamini wameshinda ngwe ya kwanza, licha ya vifo vya watu arubaini, kama ilivyokadiriwa na wataalamu wa afya.”

Huu ndio mtazamo kwa ujumla: wapinzani wa kisiasa, wakiwakilishwa hasa na muungano uitwao National Consensus Coalition (NCC), na ‘the Sudan Call Coalition’ (ambacho chenyewe ni chama cha muungano), walifanya mkutano katika makao makuu ya Chama cha Kikomunisti (the Communist Party) huko Khartoum Jumanne Decemba25, kabla ya maandamano. Walipoamua kusahau tofauti zao, walielezea dhamira yao ya kuunganisha nguvu zao, ili kupelekea “anguko la walioshikilia madaraka”

Muafaka ulifikiwa kuhusu kumuondosha al-Bashir kutoka madarakani, kuundwa kwa baraza la uraisi la mpito, na serikali ya mpito yenye watendaji ambao jukumu lao litakuwa maandalizi ya kurudia Maisha ya kisiasa yenye muundo halisi wa vyama vingi, na mwanzo wa utawala mpya. Dhumuni la makubaliano lilikuwa kuongeza mapambano, ili kulazimisha kujiuzulu kwa raisi.

Makundi yenye itikati za Kiisilamu (Islamist components) yanayounda serikali yamekumbwa na mzozano kuhusu namna ya kuitikia, baada ya kukabiliwa na uasi wa miji mbalimbali. Kujaribu kukabiliana na hali hii, walikutana Ijumaa Decemba 21.

Inasemekana kwamba, viongozi wa chama cha Harakati za Kiisilamu (Islamist movement), waliogawanyika katika mikondo inayopingana – the People’s Congress Party, inayoongozwa na Ali Al-Hajj; the al-Islah Movement, inayoongozwa na Ghazi Salahuddin Atabani; na Shura Council of the Islamic Movement, inayoongozwa na al-Islah Fateh Ezzeddine — wamekutana na Jenerali Kamal Abdul-Maarouf, mkuu wa watumishi wa jeshi.

Pamoja na kwamba hakuna uthibitisho, inasemekana pia kuwa wazo la jeshi kuchukua madaraka liliongelewa, ambalo yasemekana Abdul-Maarouf alilikubali kimsingi, na kwamba ni jambo la kujadiliana na viongozi wengine wa watumishi.

Siku hiyo hiyo, wajumbe ulikutana na Sadek al-Mahdi, kiongozi wa chama cha al-Umma na viongozi wa upinzani, ukiwemo muungano wa Sudan Call. Mkutano ambao mwenyekiti alikuwa al-Mahdi, uliandaa misingi ya majaliano ya siku za baadae kuhusu kujiuzulu kwa watendaji walioko madarakani sasa, kuudwa kwa kipindi cha mpito, na kuweka serikali ya warasimu.

Nguvu ya vijana

Hata hivyo, sababu mpya imejitokeza ambayo bila shaka itachangia muelekeo wa matukio: nguvu ya vijana, injini ya uasi maarufu katika majiji yote ya Sudan. Kizazi hiki cha vijana kilizaliwa katika kivuli cha utawala wenye itikadi zakisiasa za uisilamu na kwa hiyo wako tofauti na vizazi ambavyo vinajua vyama vya siasa vilivyokuwepo kabla ya al-Bashir.

Kimsingi, in kizazi cha uasi, kilicholelewa nje ya mazingira ya mgawanyiko wa jamii kwa mujibu wa kiitikadi za kidini na kijamii.

Vijana wengi hawazingatii mazoea ya kawaida ya utaratibu wa kujigawa kivyama na wangependa kuona harakati zinazoendelea ziende mbali zaidi ya utaratibu uliozoeleka wa kufikia makubaliano, kama vile kuacha harakati kwa kukubali mabadiliko fulani ya serikali.

Badala yake, dhamira yao ni mabadiliko ya utawala, na kuondoshwa kwa ushawishi wa kidini kwenye siasa.

Ni hii dhamira ya mapinduzi ya kweli ambayo inajitokeza katika kauli mbiu zinazoimbwa na vijana: “Uhuru, Amani, Haki.” Kwa maneno mengine, chombo chenye bidii na maamuzi thabiti sasa ni sehemu ya mustakabali wa kisiasa.

Kinaleta maono ya siku zijazo yanayotaka kuachana na tabia za kizamani, na kuunda dola ya kisasa iliyojengwa kwa misingi ya usawa, sharia, na tunu mpya za kimaadili.

Viongozi walioko madarakani sasa, hasa kwenye upinzani, ni watu wenye umri mkubwa. Vijana wanaotaka mabadiliko ya kweli watapendelea kuingia mitaani kuelezea misimamo yao ya kisiasa. Kwa hivyo, kipindi kinachokuja kitapelekea machafuko ya kisiasa makubwa zaidi, na kupelekea kwenye maamuzi magumu na hatari kubwa.

Labda wanaharakati wa kiislamu (Islamist movement) wajaribu kumshangaza kila mmoja kwa kutengeneza mapinduzi ya ikulu (ambayo bila shaka yatakabiliwa na upinzani mkubwa kutoka kwa wananchi wengi).

Ama, hivyo vikundi kadhaa vyenye itikadi za kisiasa za uisilamu vilivyokwisha kutajwa vinaweza kuunda makubaliano ya kimkatabe na wanasiasa wenye ushawishi mkubwa kama Sadek al-Mahdi, ambao wanamuelekeo zaidi wa kukubali suluhisho za kiupatanishi, ambazo zinaendana na maono yake ya kutua kwa urahisi.

Mwanzo mpya

Hii inaweza kupelekea mwisho wa utawala wa chama cha National Congress, kuanzisha kipindi cha mpito chenye Baraza lililoulioundwa na vikundi vyote vya kisiasa vya Sudan, vikiwemo vyenye itikadi za kisiasa za uisilamu, ili kujadili serikali ya namna gani itafuatia hapo baadaye.

Suluhisho hili nayo yawezekana likakataliwa na wananchi wengi, hasa vijana, na wapinzani wa muungano wa NCC.

Suluhisho linguine la tatu — ambalo ni pendeleo la wananchi wengi — ni mabadiliko ya dhati, ya kuondosha walioko madarakani wenye itikadi za kisiasa za uisilamu na kuachana na siasa za kizamani.

Suluhisho hili, la vijana na vikundi vya kimapinduzi, na ambalo lina uwezekano mkubwa wa kuipeleka Sudan kuelekea kuwa dola ya kisasa, ndio ambayo, bila shaka, itapingwa na kuzuiwa kwa nguvu zote na vikundi vya kitamaduni na kidini pamoja na wafuasi wenye itikadi za kisiasa za uislamu (Islamist movement).

Harakati ya mapinduzi inayoendelea yaweza kugongana na wanamgambo wenye itikadi za kisiasa za uisilamu (Islamist movement) ambao watachukua hatua bila kusita kutumia silaha za moto. Swali ni je, ni kwa kiasi gani askari wa jeshi na polisi hawataingilia itakapojitokeza hatari ya namna hiyo.

Je, wataingilia, kama baadhi wanavotumaini, kuunga mkono harakati ya mapinduzi na kusuluhisha mgogoro wakipendelea matakwa ya wananchi, kama ilivyokuwa mara mbili wakati wa uasi mwingine maarufu wa mwaka 1964 na 1985?

Dalili zote zinaashiria kwamba uasi wa raia wa Sudan dhidi ya watawala unazidi kukua na kuongezeka nguvu, ukionyesha dhamira wazi ya kutaka kuhitimisha utawala ulioko madarakani.

Sambamba na hilo, mazungumzo marefu yanaendelea kati ya makundi ya kisiasa yakilenga kuepuka mgogoro. Matokeo bado yako kwenye mizani.

 

 

Imetafsiriwa kwa Kiswahili na Martin Kijazi

Kwa msaada wa mapitio ya Sudanese Translators for Change – STC)

Imechapishwa kutoka orientxxi.

Imetafsiriwa kwanza kutoka makala ya Jacobin Magazine.

Tarek Cheikh ni mwandishi wa habari kutoka Sudan.

You can share this post!

Kizimbani baada ya kunaswa na kontena ya nepi feki

UHURU KENYATTA: Rais wa vitisho bila kung’ata

adminleo