Tajiri Elon Musk sasa asema anajutia makombora aliyomfyatulia Trump
WASHINGTON, AMERIKA
BILIONEA na mfanyabiashara tajiri Elon Musk Jumatano alisikitika kuhusu baadhi ya machapisho yake mitandaoni kumhusu Rais wa Amerika Donald Trump akisema hayakufaa na kukiri kwamba yalipita mipaka.
Trump alisema Jumamosi kuwa uhusiano na urafiki wake na Musk umeisha baada ya wawili hao kuanikana na kujibizana hadharani kwenye mitandao ya kijamii.
Musk ambaye anamiliki kampuni ya kifahari ya Tesla na mtandao wa X alikuwa anarejelea mswada wa ushuru na matumizi, unaopigiwa upato na Trump, kama wa aibu na utakaoumiza uchumi wa Amerika.
Musk ameyafuta baadhi ya machapisho yaliyomkashifu Trump likiwemo moja ambalo liliashiria kuwa kiongozi huyo anastahili kutimuliwa madarakani.
Duru kutoka kwa Musk, mtu tajiri zaidi ulimwenguni, zilisema kuwa hasira zake zimepungua na huenda anataka kuridhiana na Trump ili uhusiano wao urejee kama zamani.
“Ninajutia baadhi ya machapisho yangu kumhusu Rais Donald Trump wiki jana. Nilivuka mipaka sana kwa kumkabili,” akaandika Musk kwenye ukurasa wake wa X Jumatano bila kusema hasa ni chapisho lipi anajutia zaidi.
Hisa za Tesla zilipanda kwa asilimia 2.7 jijini Frankfurt, Ujerumani baada ya majibizano kati yake na Trump ambaye anaonekana kugeuka kuwa mwiba kwa viongozi mbalimbali wakuu ulimwenguni.
Musk alikuwa kati ya wafadhili wakuu wa kampeni za urais za Rais Trump mnamo 2024.
Alitumia karibu Sh38.7 bilioni katika uchaguzi huo wa Amerika.
Pia Musk anahusishwa kutumia ushawishi wake kuhakikisha kuwa Republican inatwaa viti kwenye Bunge la Kitaifa na lile la Seneti.
Trump alimtaja kama mkuu wa kitengo kilichokuwa kikiibuka na sera ya kupunguza idadi ya wafanyakazi wa serikali pamoja na matumizi ya serikali (DOGE).
Musk alijiondoa kwenye kitengo hicho cha DOGE mwezi uliopita baada ya kuukosoa mswada wa Trump ambao baadaye aliurejelea hadharani kama wenye mapendekezo yatakayokuwa ghali zaidi kuyatekeleza.
Pia alisema mswada huo ungelemaza utendakazi wa kitengo chake ambacho kilikuwa Idara ya Kuhakikisha Utendakazi na Uwajibikaji (DOGE) mufti wa serikali.
Aliposema uhusiano wao umekufa mnamo Jumamosi, Trump aliwasha moto na kumwonya bilionea huyo dhidi ya kuwafadhili wanachama wa Democrats kukataa mswada wake ambao anatarajia utaungwa mkono na Republicans.
Trump alionya kuwa atachukua hatua kali dhidi ya Musk japo hakufafanua ni hatua gani.
Pia alisema hana nia yoyote ya kuridhiana na bilionea huyo.
Jumatatu, Trump alisema hana tatizo iwapo Musk atampigia simu wala hana nia ya kusitisha mtandao wa intaneti ya angani ndani ya ikulu ya White House ambayo imekuwa ikitolewa na X yake Musk.
“Tulikuwa na uhusiano mzuri na ninamtakia kila la kheri,” akasema Trump.
Musk alionekana kupendezwa na kauli hiyo huku akijibu video kwenye X iliyoonyesha kauli za Trump, kwa ishara ya moyo.