Trump aambia Nato wamefanya ‘kosa la kijinga’ kukataa kumsaidia vitani Iran
WASHINGTON, AMERIKA
RAIS wa Amerika, Donald Trump amesema kuwa nchi yake ilifahamishwa na washirika wake wengi katika Muungano wa NATO kuwa hawataki kuingilia vita dhidi ya Iran, akisema hatua hiyo ni ‘kosa la kijinga’.
Trump alionekana kukerwa na hatua hiyo japo hakuweka wazi iwapo ataadhibu nchi hizo alizodai zimetaliki Amerika wakati muhimu kivita.
Alikuwa akizungumza baada ya kukutana na Waziri Mkuu wa Ireland Micheal Matin.
Ingawa hivyo, alitambua hiari ya nchi hizo kujitenga na vita dhidi ya Iran ambavyo vimekuwa vikiendelezwa na Amerika-Israeli.
“Nafikiri NATO wanafanya kosa la kijinga kwa sababu kila mtu anakubaliana nasi lakini hawataki kutusaidia. Sisi tunawajua na kama Amerika tutakumbuka hii kwa sababu imetushangaza sana,” akaongeza.
Alipoulizwa iwapo atalipiza kisasi dhidi ya mataifa hayo ya NATO, alisema bado hajafikiria kuhusu hilo.
Siku za nyuma Trump amewahi kutishia kuondoa Amerika kwenye NATO japo hakuzungumzia hilo wakati za ziara ya waziri huyo mkuu wa Ireland.
Trump alikuwa ametoa wito kwa mataifa hayo yasaidie kuendeleza oparesheni ya kijeshi katika Mkondo wa Strait of Hormuz ambako asilimia 20 ya mafuta ghafi ulimwenguni husafirishwa.
Iran inadhibiti Mkondo wa Strait of Hormuz na imekuwa ikitumia mashambulizi ya droni na makombora makali kulinda eneo hilo na pia kulenga Amerika-Israeli.
Washirika wa Amerika kwenye NATO walisema hawana nia kutuma meli za kivita kukabili Iran katika Mkondo wa Strait of Hormuz na kukataa ombi la msaada wa kijeshi kutoka kwa Trump.
“Kwa sababu tuna jeshi imara ambalo limeshinda vita vikali, hatuhitaji tena msaada wa NATO au mataifa wanachama wa muungano huo,” akaandika Trump katika ukurasa wake wa Truth Social mnamo Jumanne baada ya nchi za NATO kukataa ombi lake.
Vita hivyo ambavyo vilianza wiki mbili zilizopita, vinaonekana havitaisha hivi karibuni Iran na Amerika-Israeli zikishikilia msimamo mgumu.
Tayari Kiongozi mpya wa Kidini wa Iran Ayatollah Mojtaba Khamenei amesema kuwa lengo lao ni kuondoa Israeli na Amerika ulimwenguni na kulipiza kisasi kwa mauaji yote yaliyotokea Iran.
Kumekuwa na madai kuwa Urusi inasaidia Iran kwa kuipa taarifa za kijasusi.
Hata hivyo, Msemaji wa Serikali ya Urusi Dmitry Peskov Jumatano alikanusha madai hayo.
Peskov pia alikanusha kuwa Urusi inasaidia Iran na teknolojia ya droni ili kuwalenga wanajeshi wa Amerika.