Trump asitisha ghafla vita Iran saa chache kabla ya makataa ya kulipua vituo vya kawi
TEL AVIV/JERUSALEM/WASHINGTON,
Muda mfupi kabla ya tangazo hilo la ghafla la Amerika, Iran ilikuwa imeonya kuwa itashambulia viwanda vya kuzalisha kawi na maji safi katika mataifa ya Ghuba endapo Amerika itashambulia viwanda vyake vya kuzalisha umeme alivyoahidi Rais Trump.
Onyo hilo lilisababisha hofu ya kutokea kwa uhaba wa maji salama katika eneo hilo linalotegemea maji ya baharini yaliyosafishshwa kuondoa chumvi.
Mnamo Jumamosi wiki jana, Rais Trump alitoa makataa ya saa 48 kwa Iran kufungua Mkondo wa Hormuz la sivyo Amerika itashambulia viwanda vyake (Iran) vya kuzalishaji na kusambaza kawi ya umeme.
Muda huo wa makataa ulitarajiwa kutamatika Jumatatu saa moja na dakika 45 usiku.
Hali hiyo ya nipe nikupe kati ya Amerika na Iran imeendelea kutatiza masoko ya mafuta huku bei ya bidhaa hiyo ikipanda katika bara Asia.
Baada ya Amerika na Israel kuishambulia Iran kwa kipindi cha majuma matatu yaliyopita, hatua ambayo maafisa wa mataifa hayo wanasema imelemaza Iran kivita, nchi hiyo hata hivyo imeendelea kuonyesha uwezo wake wa kutekeleza mashambulio ya kulipiza kisasi.
Ndiposa, kwa mfano, mnamo Jumapili ving’ora vililia sehemu kadhaa kaskazini na kati mwa Israel, zikiwemo Tel Avivi na West Bank, vikionya kuhusu ujio wa makombora kutoka Iran.
Hata hivyo, mapema Jumatatu, Jeshi la Israel (IDF) lilisema lilianza kutekeleza msururu wa mashambulio dhidi ya miundomsingi ya Iran jijini Tehran.
Mashirika ya habari ya Iran yalisema mtoto mmoja aliuawa na watu kadhaa wakajeruhiwa baada ya kitongoji kimoja kushambuliwa kwa mabomu magharibi mwa mji wa Khorramabad.
Aidha, uharibifu ulisababishwa katika mji wa Urmia ulioko kaskazini mwa Iran, kufuatia utekelezaji wa shambulio la angani, mashirika ya habari nchini Iran yaliripoti.
Waokoaji wa Shirika la Msalaba Mwekundu nchini Iran walionekana kwenye video wakiwasaka manusura.
Hakukuwa na ripoti za watu kujeruhiwa.
Onyo la Trump lilijiri siku moja baada ya rais huyo kuashiria kuwa huenda Amerika ikasitisha mashambulio yake dhidi ya Iran.
Hii ni licha ya kwamba Meli za Kivita za Amerika zilionekana zikielekea eneo hilo la Mashariki ya Kati.
“Ikiwa viwanda vya mafuta na kawi vitashambuliwa na adui, miundomsingi yote ya kawi, teknolojia ya habari na viwanda vya kusafisha maji ya chumvi vinavyomilikiwa na Amerika na nchi za eneo hilo, vitashambuliwa kulingana na onyo la awali,” msemaji wa jeshi la Iran Ibrahim Zolfaqari aliripotiwa akisema.
Ingawa kushambuliwa kwa viwanda vya umeme kutaathiri Iran, nchi jirani zake katika eneo la Ghuba zitaathirika zaidi kwani zinatumia kawi hiyo kwa wingi.
Kwa mfano, umeme ni muhimu kwa wakazi wa miji ya nchi hizo, kwani hutumika kuendesha mitambo katika viwanda vya kusafisha maji ya chumvi, vinavyozalisha asilimia 100 ya maji yanayotumika katika mataifa ya Bahrain na Qatar.
Viwanda kama hivyo, hutumia maji ya bahari kukimu zaidi ya asilimia 80 ya maji ya kunywa nchini Umoja wa Milki ya Kiarabu (UAE) na asilimia 50 ya maji yanayosambazwa nchini Saudi Arabia.
Spika wa Bunge la Iran Mohammad Baqer Qalibaf aliongeza kuwa huenda miundomsingi muhimu na mitambo ya kawi katika eneo la Mashariki ya Kati “ikaharibiwa kabisa” endapo viwanda vya kawi vya Iran vitashambuliwa.