Kimataifa

Trump awasilisha hoja ya kuishambulia Iran katika hotuba kwa bunge la Congress

Na MASHIRIKA February 25th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WASHINGTON DC, AMERIKA

RAIS wa Amerika Donald Trump, amewasilisha kwa ufupi hoja yake kuhusu uwezekano wa kuishambulia Iran katika hotuba yake ya Hali ya Taifa mbele ya Bunge.

Trump alisema Iran inatengeneza makombora yanayoweza hata kuishambulia nchi yake huku akiirejelea nchi hiyo kama mfadhili mkubwa zaidi wa ugaidi duniani.

Katika hotuba yake ya Jumatatu, Trump alielekeza lawama kwa matendo ya Iran ikiwemo kuunga mkono makundi yenye misimamo mikali, mauaji ya waandamanaji, pamoja na programu za nchi hiyo za makombora na nyuklia kama vitisho kwa eneo hilo na kwa Amerika.

Haya yanajiri huku serikali yake ikituma wananjeshi Mashariki ya Kati karibu na Iran.

Hata hivyo rais huyo hakutoa maelezo mengi kwa wananchi kwa nini anaweza kuanzisha vita kali na Jamhuri hiyo ya Kiislamu.

Kwenye hotuba yake mbele ya wabunge, Trump alihoji kuwa, utawala wa Iran na washirika wake wameeneza ugaidi, vifo na chuki.

Na kwamba kwa sasa Iran imeanzisha tena programu yake ya nyuklia kwa lengo la kutengeneza makombora ambayo hivi karibuni yatakuwa na uwezo wa kufika Amerika.

Isitoshe Trump amedai kuwa taifa hilo linahusika na mashambulizi ya mabomu ambayo yameua wanajeshi wa Amerika na raia.

“Nia yangu ni kutatua tatizo hili kupitia njia za kidiplomasia. Lakini jambo moja ni hakika: sitaruhusu kamwe mfadhili nambari moja wa ugaidi duniani, ambaye bila shaka ndio wao, kumiliki silaha ya nyuklia. Hatuwezi kuruhusu hilo litokee,” Trump alisema kwenye hotuba yake.

Iran tayari imekanusha madai hayo ya Trump.

Kupitia ukursa wa X, msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran Esmaeil Baqaei ameandika kuwa madai ya Trump kuhusu mpango wake wa nyuklia ni ya uwongo.

Hapo awali, Iran pia ilitishia kulipiza kisasi iwapo Amerika ingeishambulia kwa makombora.

Mapema mwezi huu, waziri wa Mambo ya Nje wa Iran Abbas Araghchi alisema kwenye mahojiano yake na kituo cha televisheni Al-Jazeera kwamba Tehran haina uwezo wa kushambulia Amerika, lakini itashambulia kambi za kijeshi za nchi hiyo zilizoko Mashariki ya Kati ikiwa Washington itaishambulia.

Hotuba ya Trump kuhusu hali ya taifa pia iligusia masuala kadhaa ikiwemo uhamiaji, ushuru wa bidhaa za kimataifa, hali ya Uchumi na siasa za ndani.

Hotuba hiyo imepewa uzito mkubwa na vyombo vya habari sio tu ndani ya Amerika bali kimataifa kwa sababu, inatoa dira ya Washington kisiasa na pia kuonyesha namna utawala wa Trump ulivyojipanga kukabiliana na changamoto zinazokabili taifa hilo.