Trump: Iran isalimu amri sasa hivi, lau sivyo tutaiponda kusibaki yeyote wa kujisalimisha
BEIRUT/MIAMI/TEL AVIV/DUBAI
RAIS Donald Trump amesema hana nia ya kujadiliana na Iran, na kuzua uwezekano kwamba vita vya Iran vitaisha tu wakati jeshi na uongozi wa Tehran utakapoangamizwa kabisa.
Muda mfupi baada ya Trump kuzungumza na wanahabari ndani ya ndege rasmi ya Rais, Air Force One, Israel, mwandani wa Amerika, ilitangaza mashambulizi mapya kote nchini Iran mapema Jumapili, huku vita hivyo ambavyo vimesababisha hisia kali Mashariki ya Kati na kuvuruga masoko ya mafuta duniani vikiingia wiki ya pili.
“Wakati fulani, sidhani kutakuwa na mtu yeyote wa kusema, ‘tumesalimu amri’,” alisema Trump.
Trump ametetea operesheni kubwa zaidi ya kijeshi ya Amerika katika ukanda wa Mashariki ya Kati tangu uvamizi wa 2003 nchini Iraq, akisema Tehran ilikuwa tishio kwa Amerika pasipo kutoa ushahidi.
Amesema vilevile Iran ilikuwa karibu mno kufaulu kujenga silaha ya kinuklia.
Amerika na Israel zimejadiliana kuhusu kutuma vikosi maalum nchini Iran kutwaa madini yake ya uranium katika hatua za mwisho za vita, shirika la Axios liliripoti, likinukuu watu wanne wanaofahamu majadiliano hayo.
Alipoulizwa Jumamosi kuhusu uwezekano wa kutuma vikosi vya jeshi la ardhi kutwaa vituo vya nuklia, Trump alisema ni jambo wanaloweza kufanya “baadaye”.

Serikali za Saudi Arabia, Kuwait, Milki ya Kiarabu, na Bahrain ziliripoti mashambulizi ya droni yaliyotekelezwa na Iran katika mataifa yao Jumamosi na mapema Jumapili, huku moto mkubwa ukiteketeza jengo la afisi za serikali jijini Kuwait.
Ubalozi wa Amerika katika jiji kuu la Norway, Oslo, vilevile lilishambuliwa na mlipuko Jumapili na kusababisha uharibifu kiasi pasipo majeraha yoyote, polisi walisema.
Haikubainika papo hapo ni nini kilichosababisha mlipuko na nani alihusika.
Saudi Arabia imeambia Tehran kuwa mashambulizi yanayoendelea kutekelezwa na Iran dhidi ya milki hiyo huenda yakaisukuma Riyadh kulipiza kisasi, watu wanaofahamu suala hilo walieleza Reuters.
Kwenye jaribio la kutuliza hamaki kote eneo la Ghuba, Rais wa Iran, Masoud Pezeshkian aliomba radhi nchi jirani kwa mashambulizi yake dhidi ya vituo vya Amerika katika mataifa hayo Jumamosi.
Alipuuzilia mbali matakwa ya awali ya Trump akiitaka Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kujisalimisha kama “ndoto” lakini akasema baraza la uongozi limekubali kusitisha mashambulizi kwa nchi jirani isipokuwa pale mashambulizi dhidi ya Irani yanapotoka maeneo yao.
Matamshi ya Pezeshkian yalizua hisia mseto nchini Iran na kuilazimu afisi yake kusisitiza Iran itajibu vikali mashambulizi kutoka ngome za Amerika.
Kundi la kidini lililotwikwa jukumu la kumchagua kiongozi mpya wa kiroho Iran, kumrithi Ayatollah Ali Khamenei, aliyeuawa kwenye shambulizi wiki iliyopita lilitazamiwa kukutana Machi 8, 2026, vyombo vya habari Iran vilisema.
Sehemu kubwa ya wanachama imeafikiana kuhusu mrithi, alisema mwanachama wa Baraza la Wataalamu, Ayatollah Mohammadmehdi Mirbaqeri, kulingana na shirika la habari la Mehr.
Duru zilieleza awali kuwa huenda Mojtaba Khamenei akachaguliwa na baraza hilo la wanachama 88 kumrithi Ali Khamenei.
Milipuko mikubwa ilisikika katika sehemu za Tehran, vyombo vya habari vilisema, huku Israel ikisema ilishambulia vituo vya makombora, vituo vikuu vya kuamuru mashambulizi na vya mafuta Jumamosi.
Mashambulizi ya Amerika–Israel yamewaua raia wa Iran wasiopungua 1,332 na kuwajeruhi maelfu wengine, kulingana na Balozi wa Iran, Amir Saeid Iravani.
Israel pia ilitekeleza mashambulizi mapya dhidi ya Lebanon Jumamosi baada ya wanamgambo wa Kiislamu wanaoegemea Iran, Hezbollah, kufyatua risasi kote mpakani.
Israel ilionya Lebanon kuhusu “gharama ghali mno” ikiwa haitadhibiti wanamgambo wa Hezbollah, huku idadi ya vifo kutokana na mashambulizi ya Israel nchini Lebanon tangu Jumatatu ikipanda na kufikia 300.