Trump sasa aandama wandani wa Maduro waziri wa viwanda akinyakwa
MWANDANI wa aliyekuwa Rais wa Venezuela Nicolas Maduro alikamatwa usiku wa kuamkia Alhamisi huku Amerika ikiendelea kuwasaka marafiki wa rais huyo ambaye bado yuko kizuizini nchini Amerika.
Alex Saab, aliyekuwa waziri wa Viwanda na mfanyabiashara mwenye utata amewahi kuzuiliwa Amerika. Alizuiliwa Cape Verde muda mfupi mnamo 2020 kisha akahamishwa na kuzuiliwa Amerika kwa tuhuma za utoaji hongo kwa miaka mitatu.
Alipewa msamaha mnamo 2023 kwenye muafaka ambao raia wa Amerika waliokuwa wakizuiliwa Venezuela, waliachiliwa huru.
Vyombo vya habari Venezuela vilitoa ripoti zilizokinzana kuhusu kunyakwa kwa mfanyabiashara huyo rafiki mkubwa wa Maduro.
Baadhi ya wanahabari ambao wanaegemea upande wa serikali ya Venezuela pia walitoa ripoti tofauti kuwa Saab alikuwa amenyakwa.
Vyombo vingine vya habari vilidai Saab amejiwasilisha kwa serikali kuthibitisha kuwa kweli kulikuwa na mpango wa kumkamata.
Ingawa hivyo, Saab, 54, anatarajiwa kurejeshwa Amerika na kuzuiliwa, kwa mujiba wa afisa mmoja wa Amerika aliyeomba asinukuliwe.
Hatua hiyo itazidisha masaibu kwa watu waliotawala na Maduro ambaye alikamatwa mwezi mmoja uliopita na wanajeshi wa Amerika katika jiji kuu la Caracas.
Kwa sasa utawala wa Venezuela unashirikiana kwa karibu na Amerika chini ya Kaimu Rais Delcy Rodriguez ambaye alikuwa makamu wa Maduro.
Kabla ya kuachiliwa 2023, Saab alikuwa ameshtakiwa kwa kufyonza Sh45 bilioni za Venezuela na kuzihamishia Amerika.
Saab aliyakanusha mashtaka hayo na kukata rufaa ambayo haikuwa imeamuliwa kabla ya kupewa msamaha.
Alirejea Venezuela kwa mbwembwe nyingi huku Maduro akimrejelea kama mzalendo na hata akatuzwa kama shujaa.
Maduro baadaye alimteua Saab Waziri wa Viwanda, wadhifa ambao aliushikilia hadi mwezi uliopita alipoondolewa na Rodriguez baada ya uvamizi wa Amerika.