‘Tuko Tayari’: Iran yakaza shingo na kukataa kutii amri ya Trump
TEHRAN, IRAN
IRAN haijaonyesha dalili zozote za kutii amri ya Rais Donald Trump kuwa ifungue Mlango-bahari wa Hormuz kufikia Jumatano asubuhi au miundomsingi yake ishambuliwe na ilemazwe kabisa.
Duru kutoka Iran zilisema kuwa iko tayari kupambana na Amerika huku wakikataa pendekezo la kusitisha vita.
Iran ilisema itakubali tu kusitisha vita pale ambapo Amerika na Israel zitakoma kuwashambulia na pia ilipe fidia kutokana na uharibifu na maafa yaliyotokea.
Pia Iran ilisisitiza kuwa itaendelea kudhibiti mlango bahari huo maarufu kama Strait of Hormuz, kutoza meli zinazopita na mafuta pesa, nchi hiyo ikisema kwa sasa iko tayari kwa lolote kutoka kwa Amerika.
Trump alikuwa ametoa makataa ya Jumatano saa tisa majogoo kwa Iran iruhusu meli za mafuta zipite Strait of Hormuz la sivyo ataharibu miundomsingi na viwanda vyote vya kawi nchini humo ndani ya saa nne.
Iran ilimkejeli na kusema iko tayari kulipiza kisasi kwa kushambulia kambi za kijeshi za Amerika ukanda wa Mashariki ya Kati.
Iran ikifanya hivyo, miji mingi ya ukanda huo itasambaratika kutokana na ukosefu wa maji kwa kuwa eneo hilo ni jangwa.
Jumanne, Iran ilithibitisha kuwa hekalu moja Tehran liliharibiwa na shambulizi la Israel, tukio ambalo linaonyesha kuwa hakuna vita vitakavyositishwa.
“Hata wakati wa Pasaka bado waliendelea kutushambulia na wakalenga hekalu, eneo takatifu la kuabudu ya Wayahudi hapa Iran. Jengo hilo la kuabudu limeharibika kabisa,” akasema Hamayoun Sameh, ambaye anawakilisha Wayahudi katika Bunge la Iran.
Jeshi la Israel bado halijazungumzia tukio japo Iran ndiyo nchi ina Wayahudi wengi Mashariki ya Kati baada ya Israel. Taifa hilo lina chimbuko la Kiyahudi.
Israel nayo iliwaonya raia wa Iran wakae mbali na miundomsingi hasa ya reli nchini.
“Ukiwa karibu na treni na reli utakuwa ukihatarisha maisha yako,” Israel ikawaonya raia wa Iran.
Raia wa Iran nayo jana walikuwa wameingiwa na kiwewe kuwa nchi yao itashambuliwa.
“Natumai kuwa ni mzaha tu mwingine ambao unafanywa na Trump,” akasema Shima, 37 kutoka jiji la Isfahan
Kama raia wengine wa Iran alikuwa akitaka serikali iliyokuwepo ya Iran iondolewe ila anapinga kushambuliwa kwa miundomsingi yao.
“Hapo Amerika itakuwa imevuka mipaka na watu hawatakuwa wanaweza kujenga upya taifa lao,” akasema.
Kwenye kikao na wanahabari mnamo Jumatatu, Trump alisema kuangamiza Iran ni tukio la usiku mmoja na ni kazi rahisi sana kwake.