Kimataifa

Uingereza yawazia kuvua Andrew urithi

Na MASHIRIKA February 21st, 2026 Kusoma ni dakika: 2

SERIKALI inawazia kuanzisha sheria ya kumtoa Andrew Mountbatten-Windsor katika orodha ya urithi wa kifalme.

Waziri wa Ulinzi Luke Pollard aliambia shirika moja la habari kuwa hatua hiyo ambayo itamzuia Andrew kuwa Mfalme milele ilikuwa “jambo sahihi kufanya,” bila kujali matokeo ya uchunguzi wa polisi.

Hivi sasa, Andrew, ndugu wa Mfalme, bado yuko katika nafasi ya nane katika urithi wa kiti cha kifalme licha ya kupokonywa vyeo vyake, ikiwemo “uanamfalme,” mwezi Oktoba mwaka jana kutokana na shinikizo kuhusu uhusiano wake na mfanyabiashara ambaye ni mhalifu wa kijinsia Jeffrey Epstein.

Mnamo Alhamisi jioni, Andrew aliachiliwa huru saa 11 baada ya kukamatwa kwa tuhuma za utovu wa nidhamu katika ofisi ya umma.

Akizungumza shirika hilo la habari, Pollard alithibitisha kuwa serikali ilikuwa “dhahiri” ikishirikiana na ikulu ya kifalme kuhusu mipango ya “kumnyima nafasi ya kuwa karibu na kiti cha kifalme.”

Alisema hii ni “jambo ambalo ninatumai litaungwa na vyama vyote, lakini ni sahihi kuwa hili lifanyike tu baada ya uchunguzi wa polisi kumalizika.”

Mnamo Jumamosi, magari kadhaa ya polisi yalionekana tena yakiingia katika Royal Lodge, nyumba ya vyumba 30 ya Windsor ambapo Andrew aliishi kwa miaka mingi.

Katika moja ya hatua Ijumaa, zaidi ya magari 20 yalionekana yakiwa yameegeshwa kwenye nyumba hiyo, ingawa haijulikani kama yote yalihusiana na uchunguzi na upekuzi.

Polisi wa Thames Valley, ambao walimkamata, wanatarajiwa kuendelea na upekuzi katika Royal Lodge hadi Jumatatu.

Pendekezo la serikali linajiri baada ya baadhi ya wabunge, wakiwemo wa chama cha Liberal Democrats na SNP, kuashiria wataunga sheria kama hiyo.

Baadhi ya wabunge wa Labour ambao wamekuwa wakikosoa utawala wa kifalme walisema kuwa hawakuwa na hakika kama hatua hii inahitajika kwa sababu ni vigumu kuamini kuwa Andrew anaweza kuwa karibu na kiti cha kifalme.

Mwezi Oktoba, ofisi ya Waziri Mkuu ilisema hakukuwa na mipango ya kuanzisha sheria ya kubadilisha orodha ya warithi.

Baada ya maelezo mapya, mtaalamu wa historia David Olusoga aalisema kuwa sasa kuna “hamu kubwa ndani ya serikali na ndani ya kifalme kkutatua mgogoro huu na utawala wa kifalme kwa ujumla.”

Ikulu ya Buckingham Palace haijatoa maoni hadharani kuhusu mipango ya serikali kumtoa Andrew katika orodha ya urithi.

Hatua hii itahitaji sheria ya Bunge, ambayo itahitaji idhini kutoka kwa wabunge na majaji na itaanza kutekelezwa pale itakapopitishwa na Mfalme.

Pia itahitaji kuungwa mkono na nchi 14 za Jumuiya ya Madola ambapo Mfalme Charles III ni mkuu wa serikali, ikiwa ni pamoja na Canada, Australia, Jamaica na New Zealand.

Mara ya mwisho orodha ya urithi kubadilishwa kwa sheria ya Bunge ilikuwa mwaka 2013 wakati Sheria ya Urithi wa Ufalme ilirudisha watu ambao walikuwa wametengwa hapo awali kwa sababu walikuwa wameoa au kuolewa na Mkatoliki.

Mara ya mwisho mtu kuondolewa katika orodha ya urithi kwa sheria ya Bunge ilikuwa mwaka 1936, wakati Edward VIII na vizazi vyake viliondolewa kutokana na kujiuzulu kwake. Kiongozi wa Liberal Democrat Sir Ed Davey alisema polisi wanapaswa “kuruhusiwa kufanya kazi yao, bila woga wala upendeleo.”