Kimataifa

Vita vyachacha Iran ikipanga mswada kujiondoa mkataba wa udhibiti zana za nyuklia

Na REUTERS June 17th, 2025 Kusoma ni dakika: 1

TEL AVIV, ISRAEL

WATU wanane waliuawa jana alfajiri baada ya Iran kushambulia miji ya Tel Aviv na Haifa kwa makombora.

Makazi kadhaa yaliharibiwa katika shambulio hilo, hali iliyomfanya Waziri wa Ulinzi wa Israel kuonya kwamba raia wa Iran “watashambuliwa hivi karibuni.”

Wakati huo huo, Iran imesema bunge lake linaandaa mswada kuiwezesha kujiondoa katika Mkataba wa Kuzuia Kuendelezwa kwa Zana za Kinyuklia (NPT).

Ilisema inasalia kupinga utengenezaji wa silaha za kusababisha maangamizi makubwa.

Kupitishwa kwa mswada huo kutachukua muda wa wiki kadhaa. Inadai kuwa Israel inamiliki kiwango kidogo cha zana za nyuklia lakini haijathibitisha wala kukana madai hayo.

Israel ndilo taifa la kipekee katika eneo zima la Mashariki ya Kati ambalo halijatia saini mkataba huo wa NPT.

Jeshi la Israel, ambalo limeharibu vituo vya zana za kinyuklia vya Iran kwa mashambulio ya anga, jana lilisema limeua maafisa wanne wa kitengo cha ujasusi cha Iran, maarufu kama “Revolutionary Guards Intelligence unit”.

Utawala wa Israel ulisema jumla ya makombora saba kati ya zaidi ya 100 yaliyorushwa na Iran, yalianguka katika himaya yake.

Msemaji mmoja wa Jeshi la Ulinzi la Israel alisema kuwa Israel ilikuwa imeilemea Iran katika mashambulio ya angani na ilifaulu kuharibu vifaa vya kurusha makombora ya Iran.

Angalau watu 100 walijeruhiwa nchini Israel wakati wa shambulio hilo lililotekelezwa usiku na Iran.

Ilisemekana kuwa mashambulio hayo yalikuwa ya kulipiza kisasi, shambulio la Israel lililolenga vituo vya kinuklia na silaha za Iran.

Iran, inayokabiliwa na tishio kubwa kwa usalama wake tangu mapinduzi ya Kiislamu ya 1979, ilisema watu wanaodaiwa kuwa “wasaliti” na “majasusi” wa kusaidia Israel wamekamatwa tangu kuanza kwa vita hivyo.