Kimataifa

Waamerika sasa wachoka vita Iran, wataka visitishwe hata bila malengo kutimizwa

Na REUTERS April 2nd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WASHINGTON, Amerika

RAIA wengi wa Amerika wanaonekana kuchoshwa na vita dhidi ya Iran na wanataka vita hivyo visitishwe hata kama malengo ya taifa lao hayajatimizwa.

Kwa mujibu wa utafiti uliofanywa na Reuters/IPSOS, kwa thuluthi mbili ya raia wa Amerika, vita hivyo vinasambaratisha tu uchumi na kuwasababishia maisha magumu.

Utafiti huo ulifanywa kuanzia Ijumaa hadi Jumapili ambapo ni asilimia 27 pekee waliotaka vita hivyo viendelee hadi Amerika iyatimize malengo yake Iran.

Asilimia sita nao hawakujibu na hawaonekani kushughulishwa na vita vyenyewe.

Asilimia 40 ya wafuasi wa Republican, chama chake Donald Trump, wanataka vita visitishwe haraka huku asilimia 57 wakitaka vita vidumu kwa kipindi kirefu mradi tu maslahi ya Amerika yanatimizwa.

Vita hivyo vya tangu Februari 28 vimeenea Ukanda wa Mashariki ya Kati, maelfu wakiuawa.

Uchumi wa ulimwengu pia umeathirika huku bei ya kawi ikipanda pamoja na mfumko wa uchumi kushuhudiwa.

Katika utafiti huo, asilimia 60 ya raia wa Amerika walisema hawakuunga hatua ya nchi yao kuingia vita na kushambulia Iran huku nao asilimia 35 wakisema vita hivyo vilistahili.

Utafiti huo ulishirikisha raia 1,021 wa Amerika.

Takwimu zinaonyesha kuwa kati ya athari ya vita hivyo ni kupanda kwa gharama ya kawi huku wengi wakitarajia kuwa hali itakuwa mbaya zaidi iwapo vita hivyo havitakoma.

Hata asimia 40 ya wafuasi wa Republicans, walilalamika kuwa bei ya juu ya kawi imeanza kuwaathiri na kama vita vyenyewe vitaendelea kwa mwaka mmoja zaidi, uchumi wa Amerika utakuwa pabaya zaidi.

Kutakuwa na uchaguzi wa katikati mwa muhula Novemba ambapo Republicans na Democrats watatifuana na vita hivyo vinatumiwa na pande zote mbili kujipigia debe.

Trump atakuwa akilenga kuendelea kudhibiti Bunge la Congress na lile la Seneti.

Mara nyingi kwenye chaguzi za nyuma, chama tawala kimekuwa kikipoteza idadi yake kwenye Bunge la Congress kutokana na sera zake za uongozi.

Huku raia wa Amerika wakichoka, Iran inaendelea kukaa ngumu licha ya kuibuka kuwa mazungumzo yanakumbatiwa kumaliza vita hivyo.

Pia Iran imefunga mlango bahari maarufu wa Strait of Hormuz na inaruhusu tu mataifa washirika wake kama China kupitisha meli zake za mafuta katika eneo hilo.

Baada ya kuuawa kwa viongozi wake serikalini na wakuu wa jeshi, Iran inaonekana haichangamkii mazungumzo kati yake na Amerika huku ikiendeleza uhasama dhidi ya Israel.