Kindiki njia panda uchaguzi wa 2027 ukikaribia ODM kikinyemelea wadhifa wake
NAIBU wa Rais Profesa Kithure Kindiki sasa anajikuna kichwa kutokana na maamuzi magumu ambayo huenda yakamjenga au kumbomoa kisiasa kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.
Profesa Kindiki anakabiliwa na uamuzi wa kuendelea kumuunga mkono Rais William Ruto na wakati huo huo kupoteza wadhifa wake ambao sasa unanyemelewa na ODM.
Kitakwimu kura ambazo ODM inaleta katika kapu la Rais Ruto ni nyingi ikilinganishwa na zile za Profesa Kindiki kutoka Mlima Kenya, eneo ambalo sasa linaonekana limeasi serikali.
Mawimbi kama haya yanaweza kulinganishwa na mtikiso ambao ulimkumba Profesa Kindiki wakati ambapo Rais Ruto alikuwa akimchagua mgombeaji mwenzake wake kuelekea uchaguzi mkuu wa 2022.
Wakati huo Profesa Kindiki alitangaza kuwa amestaafu siasa lakini baada ya utawala wa UDA kushinda kura, alikubali uteuzi wa Rais Ruto kama waziri wa usalama wa ndani.
Wiki jana akiwa Kaunti ya Kirinyaga, Profesa Kindiki alionekana kama aliyeanza kusalimu amri kuhusu kudumisha wadhifa wake aliposema nafasi za uongozi si za kushikiliwa milele.
“Kile ambacho ni muhimu ni jambo unalolifanya ukiwa afisini kwa sababu nafasi huja na kuenda. Kuna maisha baada ya siasa na utumishi wa umma,” akasema Profesa KindikiKwa mujibu wachanganuzi wa kisiasa, hali ambayo Profesa Kindiki amejipata ni ngumu hasa ikizingatiwa ODM inanyemelea nafasi yake.
“Hicho kiti si cha kutengewa mtu mmoja, ni cha umma. Ni kati ya matakwa ambayo tunalenga kuhakikisha tunayatimiza kulingana na makubaliano yetu na Rais William Ruto,” akasema Dkt Oburu Oginga, Kiongozi wa ODM.
Mchanganuzi wa Masuala ya kisiasa Profesa Munene Nyaga anasema kuwa kibarua kwa naibu rais ni kuwa alitegemea kutumia kura za Mlima Kenya kuendelea kuwa naibu wa Rais Ruto ila kupata kura hizo sasa kunaonekana kama jambo lisiloweza kutimia.
“Kindiki aliteuliwa kuhakikisha kura za Mlima Kenya zinasalia upande wa serikali lakini hilo hadi sasa linaonekana kuwa ngumu. Pia kulikuwa na dhana kwamba Rigathi Gachagua angeisha kisiasa ila sasa ndio ameteka nyoyo za wakazi wa mlimani ambao hawajaridhishwa na utawala wa sasa,” akasema Profesa Nyaga.
Kibarua kingine ni wito wa baadhi ya wabunge wa Mlima Kenya kuwa Rais Ruto ameteua Gavana wa Kirinyaga Anne Waiguru kuwa mgombeaji mwenza wake kuhakikisha usawa wa kijinsia.
“Profesa Kindiki amehudumu kama seneta kwa mihula miwili na naibu rais. Bi Waiguru anamaliza muhula wake wa pili na anatosha kuwa mgombeaji mwenza,” akasema Mbunge huyo mnamo Aprili 2, 2026 akiwa Kaunti ya Murangá.
Wengine wanapendekeza akubali kupoteza nafasi yake na kuwa waziri kwenye serikali ijayo.Naye mchanganuzi Malila Munywoki anapendekeza ahame na kujiunga na mrengo wa Bw Gachagua kumzima kabisa Rais Ruto Mlima Kenya.