Habari

Korti yaamua kuwa ndoa si biashara itumiwe kupata mali

Na SAM KIPLAGAT February 8th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MAHAKAMA Kuu imepuuza jaribio la mwanamke kudai nusu ya mali aliyodai kuwa ni ya aliyekuwa mume wake, baada ya jaji kuamua kuwa alishindwa kuthibitisha kuwa mali hiyo ilikuwa ya ndoa.
Jaji Reuben Nyakundi alisema mahakama haiwezi kuchunguza mchango wa upande wowote katika upatikanaji wa mali iwapo umiliki wa mali yenyewe haujathibitishwa.
Mwanamke huyo, aliyetambuliwa kama VJM kwa sababu za kisheria, alikuwa akiomba mgao sawa wa mali aliyodai ilimilikiwa na aliyekuwa mume wake, KKM.
Hata hivyo, jaji alitupilia mbali kesi hiyo na kusisitiza kuwa ndoa haipaswi kuchukuliwa kama muamala wa kibiashara pale inapovunjika.
Mahakama ilibainisha kuwa licha ya kuorodhesha mali, mlalamishi hakuwasilisha hata hati moja ya umiliki au stakabadhi yoyote kuthibitisha madai yake.
“Kwa kuzingatia kuwa kuna mali 33 inayolengwa katika kesi hii na mlalamishi hajawasilisha hata hati moja ya umiliki, mahakama hii haiwezi kuamua iwapo mali hiyo inapaswa kugawanywa kati ya wahusika,” mahakama ilisema.
Mahakama ilisisitiza msimamo wa kisheria kuwa mali iliyopatikana kabla ya ndoa inabaki kuwa ya aliyeipata. Hata hivyo, endapo thamani ya mali hiyo itaongezeka wakati wa ndoa kutokana na mchango mkubwa wa mwanandoa mwingine, basi haki ya manufaa inaweza kuibuka.
Jaji alieleza kuwa kanuni inayoongoza kesi kama hizi ni kwamba usawa haumaanishi lazima ugavi uwe sawa, na kila kesi lazima ichunguzwe kulingana na mazingira yake.
Jaji Nyakundi aliongeza kuwa ndoa haifuti haki binafsi za wanandoa, na kila mmoja ana uhuru wa kumiliki mali kivyake. Si kila mali inayomilikiwa na mmoja wao huchukuliwa moja kwa moja kuwa mali ya ndoa.
Alisisitiza kuwa madai kama hayo lazima yaungwe mkono na ushahidi wa wazi wa mchango, iwe wa kifedha au usio wa kifedha.
Katika kesi hii, mahakama ilipata kuwa hakukuwa na ushahidi wa kuaminika kuonyesha kuwa mlalamishi alichangia kupatikana au kuboreshwa kwa mali aliyoorodhesha.
Hivyo basi, hakukuwa na msingi wa kudhani kuwa mali hiyo ilimilikiwa kwa pamoja kwa sababu tu wahusika walikuwa wameoana.
Mwanamke huyo aliambia mahakama kuwa alifunga ndoa na mshtakiwa Septemba 12, 2008, na kuwa katika kipindi cha ndoa walipata mali kadhaa kwa pamoja, ikiwemo nyumba ya ghorofa aliyodai ilinunuliwa mwaka 2012 kwa Sh25 milioni.
Aidha, alidai walijenga nyumba ya ndoa na kuishi katika nyumba nyingine za makazi mjini Eldoret.
VJM alisema alitoa mchango mkubwa wa moja kwa moja na usio wa moja kwa moja, na kuwa aliyekuwa mume wake alishikilia mali kwa niaba yake.
Alisema pia ndoa yao ilivunjwa rasmi kupitia amri ya mahakama iliyotolewa Juni 7, 2024, na akaiomba mahakama impe mgao sawa wa mali ya ndoa.
Hata hivyo, mwanaume huyo alipinga madai hayo.
Ingawa alikiri kufunga ndoa mwaka 2008, alidai ndoa ilianza kuyumba mapema kutokana na ukatili.
Alimshtumu mlalamishi kwa kutofichua taarifa kamili, akisema alikuwa na watoto kutoka uhusiano wa awali, jambo lililoathiri imani yao.