Habari

Maaskofu kwa Ruto: Vunja DCI kabla Kenya isambaratike

Na ALEX ODHIAMBO June 22nd, 2025 Kusoma ni dakika: 2

MAASKOFU wa Kanisa la Kianglikana (ACK) kutoka eneo la Nyanza wametoa wito mkali kwa Rais William Ruto kuvunja mara moja Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI), wakiilaumu kwa mauaji ya kiholela, kupotea kwa raia kiholela, na matumizi mabaya ya nguvu na polisi.

Wakizungumza katika kanisa jipya la ACK St. Stephen’s jijini Kisumu, maaskofu hao walisema DCI imekuwa “kitengo cha kuzua hofu wala si tena cha kuchunguza uhalifu”.

Wakiongozwa na Askofu wa Dayosisi ya Maseno Kusini, Charles Ong’injo, walieleza masikitiko yao kwa ukatili unaofanywa na polisi, hususan baada ya mauaji katili ya mwalimu na bloga Albert Ojwang aliyedaiwa kuteswa na maafisa wa DCI.“Wakati umefika wa kuvunjwa kwa DCI.

Kimekuwa chombo cha hofu kinachotumiwa na wenye mamlaka kukandamiza raia. Hakuna tofauti kati ya DCI na magenge ya uhalifu yanayotisha wananchi,” alisema Askofu Ong’injo.

Maaskofu kutoka Siaya, Kisii, Homa Bay, Migori na Kisumu waliunga wito huo wakisema DCI imepoteza mwelekeo na heshima, na yafaa kuvunjwa.

“DCI si chombo cha kuchunguza uhalifu tena bali ni cha kuzalisha hofu,” aliongeza Askofu Prof David Kodia wa Dayosisi ya Bondo ambaye pia ni mwenyekiti wa maaskofu wa ACK Nyanza.

Aidha, viongozi hao wa dini walilaani vikali ukatili dhidi ya waandamanaji jijini Nairobi na kumlaumu Gavana Johnson Sakaja kwa madai ya kufadhili magenge ya kuvuruga maandamano.

“Ni wazi kuwa katika vurugu za hivi majuzi jijini Nairobi mwanasiasa alilipa wahuni kuvuruga maandamano ya amani. Hadi leo hajachukuliwa hatua,” alidai Ong’injo.

Vongozi hao wa kanisa walimtaka Rais Ruto kuvunja kimya chake na kushughulikia haraka utovu wa nidhamu katika idara za usalama.

“Tumechoka. Rambirambi hazitoshi. Wakenya wanataka haki si maneno ya kuwafariji,” aliongeza.

Pia walionya maafisa wa polisi wakome kuwa chanzo cha hofu kwa raia. “Wako vijana wengi wasio na kazi wanaoweza kuchukua nafasi za maafisa wa polisi waliopo. Iwapo hali hii haitarekebishwa wananchi wataanza kujihami wenyewe, na hapo ndipo taifa litapotea kabisa,” alionya Ong’injo.

Kwa mujibu wa maaskofu hao, taasisi kama IPOA (Mamlaka Huru ya Kuchunguza Utendakazi wa Polisi) imeshindwa kutimiza wajibu wake:
 “IPOA ni mbwa asiye na meno, huzungumza sana lakini hana uwezo wa kuchukua hatua yoyote,” alisema Askofu Ong’injo.

Walitahadharisha kuwa ukatili wa polisi unaendelea kuchochea hasira na msimamo mkali miongoni mwa vijana, jambo linaloweza kusababisha uasi mkubwa wa kiraia.

“Kama kanisa, hatutakaa kimya. Tutaomba, tutazungumza, na tutasimama na watu,” alisisitiza Askofu Kodia.

“Mungu hakuwaita maaskofu kubariki ukatili.”Wito huo kutoka kwa viongozi wa kiroho unajiri wakati ambapo Kenya inazidi kukumbwa na hali ya sintofahamu, ukatili wa maafisa wa usalama na hasira.