Habari

MAHAKAMA: Una haki ya kulea mtoto wako hata kama hujalipa mahari

Na JOSEPH WANGUI April 13th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KATIKA familia nyingi za Kenya, mahari ni ishara ya ndoa, heshima na utamaduni.

Hata hivyo, katika kesi ya hivi karibuni ya kisheria kuhusu ulezi wa mtoto, mahari iligeuka kuwa kitu tofauti kabisa yaani kizuizi kwa baba kumchukua binti yake mwenyewe.

Kesi hiyo ya miaka tisa imeibua maswali kadhaa kuhusu ni nani huamua hatima ya mtoto pale mila na haki za kikatiba zinapokinzana.

Kiini cha mzozo huo kilikuwa msichana aliyezaliwa mwaka 2014, muda mfupi kabla ya mama yake kufariki wakati wa kujifungua.

Baada ya tukio hilo la kusikitisha, babu na nyanya wa upande wa mama walimchukua na kumlea tangu utotoni.
Rekodi za mahakama zinaonyesha kuwa baba yake hakutoweka.

Aliendelea kuchangia malezi ya mtoto kwa kutuma pesa mara kwa mara, kutoa chakula na mahitaji ya msingi pamoja na kumwekea bima ya matibabu.

Pia aliajiri mfanyakazi wa nyumbani kusaidia malezi na aliendelea kumtembelea mtoto, kuhudhuria sherehe zake za siku ya kuzaliwa na kushiriki katika maisha yake.

Hata hivyo, kadri miaka ilivyopita, mvutano ulianza kujitokeza kati ya familia hizo mbili.

Baba alipodai ulezi kamili, babu na nyanya walipinga vikali hatua hiyo, na mzozo huo ukaishia mahakamani, kutoka Mahakama ya Watoto ya Kerugoya mwaka 2017 hadi Mahakama Kuu mwaka 2020, na hatimaye Mahakama ya Rufaa ya Nyeri mwaka 2023, iliyotoa uamuzi wiki iliyopita.

Kiini cha mgogoro huo hakikuwa tu malezi.

Babu na nyanya walidai kuwa baba huyo hakutimiza masharti ya kimila, hasa kulipa mahari kikamilifu na kukamilisha taratibu za kitamaduni kama vile kutambulisha familia.

Walisisitiza kuwa bila hatua hizo, hakuwa na haki ya kuchukua mtoto.

Kwa upande wake, baba aliambia mahakama kuwa alijaribu kutatua mzozo huo kwa kushirikisha wazee wa kijamii na hata kulipa baadhi ya madai ya mahari.

Hata hivyo, alidai kuwa masharti yaliendelea kuongezwa na hatimaye akazuiwa kuchukua mtoto.

Alieleza pia kuwa ameoa tena na ana mtoto mwingine, akisisitiza kuwa binti yake angepata fursa ya kukulia katika familia yenye upendo wa mama na uwepo wa ndugu.

Awali, Mahakama ya Watoto iliamua kuwa mtoto aendelee kulelewa na babu na nyanya hadi atakapofikisha miaka 11, huku baba akipewa haki ya kumtembelea.

Lakini Mahakama Kuu ilibatilisha uamuzi huo na kumpa baba ulezi kamili kama mzazi aliyesalia.

Babu na nyanya walikata rufaa, lakini Mahakama ya Rufaa ilitupilia mbali madai yao na kuthibitisha uamuzi wa Mahakama Kuu.

Majaji walibainisha kuwa pande zote mbili zilionyesha kujali ustawi wa mtoto, lakini wakasisitiza kuwa maslahi ya mtoto ndiyo ya kipaumbele.

Walieleza kuwa mtoto anahitaji baba, babu na nyanyl akini uhusiano huo unapaswa kuwa wa kusaidiana, si wa kushindana.

Mahakama ilisisitiza kuwa kwa mujibu wa Katiba na Sheria ya Watoto, jukumu la mzazi ni la baba na mama, bila kujali ndoa au mila. Ilieleza wazi kuwa mila haiwezi kuzidi haki ya mtoto.

Aidha, mahakama haikupata ushahidi wowote unaoonyesha kuwa baba huyo hafai kulea mtoto.

Kinyume chake, ilibaini kuwa ana uwezo wa kumpa mtoto mazingira bora ya kukulia.

Hoja ya babu na nyanya kuwa mtoto amezoea kuishi nao haikutosha kubatilisha haki ya baba.

Mahakama ilisema mtoto hapaswi kunyimwa upendo na malezi ya mzazi wake aliyebaki bila sababu za msingi.