Majambazi wavamia kituo cha polisi, kumuua afisa na kuiba bunduki
POLISI katika Kaunti ya Kakamega wanasaka genge la wahalifu walioshambulia kituo cha polisi cha Nyalenya, Mumias Magharibi wakaua afisa mmoja na kuiba bunduki.
Katika shambulio hilo lililofanyika Ijumaa usiku, maafisa wengine wawili walipata majeraha mabaya. Mke wa mmoja wa maafisa wa polisi pia alijeruhiwa na amelazwa katika hospitali moja ya kaunti ya Bungoma.
Wavamizi walifika katika kituo hicho cha polisi kwa pikipiki mbili na kudai walitaka kuripoti wizi wa pikipiki kabla ya kutekeleza shambulio la kikatili.
Kwa mujibu wa chanzo cha polisi, wavamizi walishambulia ghafla na kuacha maafisa wa polisi wakiwa na majeraha makubwa kabla ya kutoroka na bunduki mbili aina ya G3, kila moja ikiwa imejaa risasi.
“Shambulizi lilifanyika ghafla na kwa kutumia silaha, na maafisa wa polisi walibaki na majeraha makubwa,” chanzo cha polisi kilieleza.
Familia ya afisa aliyeuawa, Richard Utolo ilikuwa na huzuni.
Ndugu yake, Gabriel Utolo, alisema walipokea taarifa za kifo cha Richard kwa masikitiko makubwa. “Alishambuliwa na akafariki akipelekwa hospitalini Bungoma usiku.
Alikuwa kama baba yetu,” alisema Gabriel.
Viongozi wamehimiza serikali kuimarisha usalama hasa katika vituo vya polisi vilivyo vijijini. Msako wa kutafuta bunduki zilizoibwa unaendelea, huku polisi wakichunguza kiini cha shambulio hilo.