Mambo yako shwari sasa JKIA- KAA yasema
SHUGHULI za kawaida zimerejea katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Jomo Kenyatta (JKIA) baada ya kusitishwa kwa muda mapema Alhamisi Oktoba 16, 2025.
Kwenye taarifa mwendo wa saa nane alasiri, Mamlakaya Kusimamia Viwanja vya Ndege Nchini (KAA) ilithibitisha kuwa safari za ndege zimerejelea kama kawaida na kuwahakikishia wananchi kwamba usalama umewekwa.
“Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Jomo Kenyatta (JKIA) sasa umefunguliwa kwa shughuli za kawaida baada ya kufungwa kwa muda mapema leo (Alhamisi),” Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa KAA Mohamud Gedi akasema.
Aliwashauri wasafiri, ambao safari zao zilikuwa zimeratibiwa wakati shughuli zilipositishwa, kuwasiliana na mashirika husika ya ndege kwa maelezo kuhusu safari zao.
KAA iliwashukuru wasafiri, mashirika ya safari za ndege na umma kwa ujumla kwa uvumilivu wao wakati shughuli zilisitishwa kwa muda katika JKIA.
“Tumejitolea kutoa huduma bora za usafiri na huduma nyinginezo katika JKIA kwa njia bora,” Bw Gedi akaeleza.
Awali, majira ya asubuhi, Mamlaka ya Kusimamia Safari za Angani (KCAA) ilisitisha shughuli kwa muda katika uwanja wa JKIA baada ya waombolezaji kuvuruga usalama humo wakati kuwasili kwa mwili wa Hayati Raila Odinga.
Kwenye taarifa kwa vyombo vya habari mamlaka hiyo ilisema ililazimika kuchukua hatua hiyo baada ya waomboleza kuingia sehemu zisizoruhusiwa katika uwanja huo.
“KCAA inajulisha umma kwamba shughuli katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Jomo Kenyatta zimesitishwa kwa muda kutokana na hali ya usalama iliyoshughuhiwa kufuatia kuwasilisha kwa mwili wa Mheshimiwa Raila Odinga,” akasema Mkurugenzi Mkuu wa KACC Emile Arao.
Mamlaka hiyo ilitoa wito kwa umma na wasafiri kusalia watulivu na kutofika katika uwanja huo wa ndege hadi mwelekeo utakapotolewa baadaye.
“Shughuli za kawaida zitarejelewa kama kawaida baada ya uwanja wa JKIA kutawazwa kuwa salama,” Bw Arao akasema.
Ndege ya Shirika la Ndege Nchi (KQ) iliyobeba mwili wa Raila ilipowasili katika uwanja huo, maelfu ya waombolezaji walionekana kuwalemea maafisa wa vikosi mbalimbali vya usalama.
Isitoshe, baadhi yao, waliokuwa wakilia kwa sauti wakibeba matawi, walionekana karibu zaidi na ndege hiyo iliyopewa jina “RAO OO1”.