Habari

Marehemu Ng’eno ‘alitabiri’ kifo chake akila na wenyeji

Na VITALIS KIMUTAI March 7th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MAREHEMU Mbunge wa eneo la Emurua Dikirr, Johana Ng’eno aliyezikwa jana, alitoa kauli ambazo ziliashiria alitabiri kifo chake alikula pamoja na wakazi wa eneo bunge lake usiku uliotangulia kabla ya ajali ya helikopta kumuua pamoja na watu wengine watano.
Mbunge huyo mwenye msimamo mkali wa chama cha United Democratic Alliance pia alionekana kana kwamba alikuwa na maono kuhusu kifo chake.
Mara kwa mara, aliwaambia wafuasi wake katika mikutano mbalimbali katika Bonde la Ufa kwamba, kifo ni jambo lisiloepukika kwa kila binadamu.
Waathiriwa wa ajali ya helikopta iliyotokea Februari 28, 2026 katika kijiji cha Chepkiep, eneo bunge la Mosop katika kaunti ya Nandi ni pamoja na Mbunge Ng’eno, rubani George Were, mwanahabari mpigaji picha Nick Kosgei, afisa wa Huduma ya Misitu Kenya Amos Kipngetich Rotich, mwalimu Carlos Robert Kibet Keter, na afisa wa itifaki wa serikali ya kaunti ya Narok Wycliff Kiprotich Rono.
Waziri wa Usalama wa Ndani Kipchumba Murkomen alisema wakati wa ibada ya wafu iliyofanyika katika AGC Karen Church kwamba, imani ya Ng’eno kwa Mungu ilikuwa kubwa kuliko ilivyodhaniwa na wengi.
“Wimbo wake alioupenda sana ulikuwa wimbo wa Kalenjin nambari 100 Miten Emet Barak (kuna makao mbinguni). Nafikiri alikuwa akidumisha mawasiliano ya karibu na Mungu,” alisema Murkomen alipomwomboleza mbunge huyo ambaye wakati mwingine walitofautiana kisiasa.
Mkutano uliofanyika katika kijiji cha Changina, wadi ya Elkerin uliendelea hadi saa nane za usiku. Katika mkutano huo, mbunge huyo alieleza kwa kina mafanikio aliyopata katika mihula yake mitatu bungeni na mipango ya maendeleo aliyokuwa nayo kwa wakazi wake.
Msaidizi wake binafsi Bernard Ngeno alisema bosi wake alikuwa katika hali nzuri kabisa siku hiyo.
Kwa mujibu wa Ngeno, mbunge huyo aliwaambia wakazi mara kadhaa kwamba, atawaacha mikononi mwa Rais William Ruto na Gavana wa Narok Patrick Ntutu kauli ambayo sasa inaonekana kama ishara ya kuwa alihisi kifo chake kinakaribia.