Habari

Milio ya risasi polisi wakikabili waandamanaji katikati ya jiji

Na BENSON MATHEKA June 25th, 2025 Kusoma ni dakika: 1

MILIO ya risasi imechana anga polisi wakikabili waandamanaji katikati ya jiji la Nairobi huku ikiripotiwa kuwa afisa wa polisi alijeruhiwa katika tukio ambalo waandamanaji walilemea maafisa wa usalama.

Vijana wamekuwa wakikabiliana na polisi tangu saa tatu na nusu asubuhi  serikali ikilenga kuzima maandamano,

Milio ya risasi ilisikika katika barabara ya Moi Avenue ambako mfanyabiashara wa barakoa alipigwa risasi kichwani katika maandamano ya wiki jana.

Kufikia sasa hakuna ripoti za majeruhi wa risasi japo watu kadhaa wanasemekana kutibiwa katika kiliniki moja katika msikiti wa Jamia.

Vijana wamekuwa wakitawanywa na kisha kukusanyika kwa nguvu na kurejea barabarani kuendelea kuimba wakitaka haki kwa wenzao waliouawa kwenye maandamano mwaka jana.

Milio ya risasi imejiri huku milipuko mikubwa ikisikika katikati ya jiji la Nairobi polisi wakifyatulia vitoa machozi waaandamanaji wanaoadhimisha kuuawa kwa vijana zaidi 60 mwaka jana wakipinga mswada wa fedha 2024.

Maandamamo hayo yanaendelea katika miji zaidi ya 16 kote nchini. Vijana wamemiminika katikati ya jiji licha polisi kuweka vizuizi kuthibiti magari na wanaoingia jijini.

Wakati mmoja waandamanaji walijaribu kuvamia kituo cha polisi cha Central lakini wakatawanywa kwa vitoa machozi. Maandamano yamechacha Githurai, Kitengela, Mlolongo, Nyeri, Nakuru, Karatina,Mombasa, Nyahururu, Wote miongoni mwa miji mingine.

Shughuli zote zimesimama katikati ya miji na mitaa ambako wakazi wanaandamana