Habari

Mshukiwa mmoja wa ulanguzi wa dawa za kulevya anaswa Nairobi

Na WINNIE ONYANDO March 1st, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MSHUKIWA mmoja wa ulanguzi wa mihadarati amenaswa jijini Nairobi kufuatia operesheni iliyoendeshwa na polisi katika nyumba moja ya makazi inayodaiwa kutumika kuhifadhi na kusambaza dawa hizo za kulevya.

Shirika la Huduma za Polisi (NPS), kwenye taarifa lililotoa Jumapili, Machi 1, 2026, kupitia akaunti yake ya mtandao wa X, lilisema kuwa maafisa wake kutoka Kituo cha Polisi cha South B, walitekeleza uvamizi katika kitongoji cha Sana Sana, karibu na mtaa huo, baada ya kupashwa habari kwamba biashara hiyo haramu ilikuwa ikiendeshwa katika makazi hayo.

“Maafisa kutoka Kituo cha Polisi cha South B waliendesha msako katika eneo la Sana Sana baada ya kupokea taarifa za kijasusi kwamba nyumba moja ya makazi ilikuwa ikitumia katika kituo cha uhifadhi na usambazaji wa dawa za kulevya,’’ NPS ikasema.

Baada ya kuvamia makazi hayo, polisi waliwakamata mshukiwa mmoja anayesemekana kuwa raia wa kigeni, aliyepatikana ndani ya chumba moja.

Walipoendelea na msako zako zaidi, kulingana na taarifa hiyo ya NPS, maafisa wa polisi walipata misoko 316 ya bangu na sachet za poda nyeupe zinazoshukiwa kuwa dawa za kulevya.

Vitu hivyo, vitafanyiwa uchunguzi kubaini ikiwa vinasheheni kemikali zinazohusishwa na dawa za kulevya.

“Aidha, maafisa walipa pesa za kigeni zinazoshukiwa kutokana na biashara hiyo haramu.

Mshukiwa huyo, ambaye jina lake halikutambuliwa, anazuiliwa katika korokoro ya kituo cha polisi cha South B huku polisi wakiendelea kuwasaka washirika wake, kabla ya kuwasilishwa kwake kortini.