Habari

Mwanamume afariki kwa majeraha ya risasi aliyopata akiandamana

Na PIUS MAUNDU Na BENSON MATHEKA June 25th, 2025 Kusoma ni dakika: 1

MTU mmoja alifariki baada ya kupigwa risasi na polisi maelfu ya waandamanaji walipoingia barabarani kote nchini kukumbuka vijana waliouawa katika maandamano ya kupinga Mswada wa Fedha 2024.

Polisi walisema mtu huyo alipigwa risasi katika mji wa Matuu, Kaunti ya Machakos. Msimamizi wa hospitali ya  kaunti ndogo ya Matuu Bw Julius Makau alisema  hospitali hiyo ilipokea wagonjwa tisa waliokuwa wamejeruhiwa baada ya polisi kufyatua risasi kwa waandamanaji waliokuwa wakichoma matairi na kujaribu kuvamia Kituo cha Polisi cha Matuu.

“Wagonjwa sita walikuwa na majeraha ya risasi. Mwanaume aliyefariki alipigwa risasi tumboni. Tuna mwingine ambaye hali yake ni mahututi baada ya kupigwa risasi kichwani. Wagonjwa wengine watatu walipata majeraha madogo yaliyochangiwa na mambo mengine,” alisema Bw Makau.

Maelfu ya vijana walimiminika barabarani katika miji  tofauti nchini kuadhimisha mwaka mmoja tangu vifo vya waandamanaji waliouawa wakipinga serikali mwaka jana.

Jijini Nairobi, maandamano yalichacha, huku polisi wa kukabiliana na ghasia wakirusha vitoa machozi kuwatawanya waandamanaji waliokuwa wamejaa katika barabara kuu za katikati ya jiji kama Moi Avenue, Kenyatta Avenue na Kimathi Street.