Natembeya ajitangaza kigogo wa Mulembe akiapa kuangusha Musalia, Weta
GAVANA wa Trans Nzoia George Natembeya Jumatatu alianza mikakati ya kuwaengua Musalia Mudavadi na Moses Wetangúla kama vigogo wa siasa za Magharibi akijitangaza kuwa mwenye usukani wa uongozi miongoni mwa jamii ya Waluhya.
Bw Natembeya alilakiwa na halaiki ya raia kwenye miji ya Chavakali, Mbale, Kakamega, Malava, Webuye kisha kupewa makaribisho ya aina yake nyumbani kwake mji wa Kitale.
“Enzi ambapo Waluhya walirejelewa kama askari gongo zimepitwa na wakati. Tuko hapa kupigania eneo letu ambalo lina idadi tosha ya watu ya kuongoza nchi,” akasema Bw Natembeya akihutubia umati mkubwa mji wa Kakamega ambao huchukuliwa kama makao makuu ya siasa za jamii ya Mulembe.
Hii ilikuwa mara ya kwanza ambapo Bw Natembeya alikuwa akirejea Magharibi tangu anyakwe wiki jana na makachero wa Tume ya Maadili na Kupambana na Ufisadi kisha kufikishwa mahakamani kwa makosa ya ufisadi.
Alishtakiwa kwenye kesi ya uporaji wa Sh3.2 milioni kupitia tenda za kaunti, mashtaka aliyoyakanusha na akawaachiliwa kwa pesa taslimu Sh500,000. Pia alipigwa marufuku kukanyaga afisi za kaunti kwa siku 60.
Akiwa ameandamana na madiwani kadhaa na Kiongozi wa chama cha Roots George Wajackoya, Bw Natembeya alisema kuwa hatatereka na vuguvugu lake la Tawe litabadilisha siasa za Magharibi.
Pia alikariri kuwa atahakikisha jamii ya Mulembe inaheshimiwa nchini na inatumia idadi yao kuamua mkondo wa siasa nchini.
Bw Mudavadi ambaye ni Kinara wa mawaziri na Bw Wetangúla, Spika wa Bunge la Kitaifa, wamekuwa wakichukuliwa kama mibabe wa siasa za Magharibi kutokana na nyadhifa zao serikalini.
Kando na wawili hao, Kinara wa ODM Raila Odinga amekuwa na ushawishi wa kisiasa Magharibi huku eneo hilo likimuunga mkono kwa dhati kwenye chaguzi za 2007, 2013, 2017 na 2022.
Eneo la Magharibi halijakuwa na umoja ambao ulikwepo enzi za vigogo wa upinzani marehemu Kijana Wamalwa na Masinde Muliro.
Bw Natembeya alisema masaibu yake ya wiki jana hayatamteteresha huku akisema yuko tayari kukabiliana na Kenya Kwanza ambayo imetelekeza Magharibi.
“Nataka niwaambie kuwa hakuna vitisho ambavyo vitaniyumbisha. Siwezi kukaa wakati watu wetu wanateseka kutokana na ukosefu wa kazi, umaskini na kutosoma. Ndoto yangu ni kuhakikisha wanajitegemea na kujihimili katika kila kitu,” akaongeza.
Bw Wajackoya naye alishutumu utawala wa Rais William Ruto kwa kumhangaisha Bw Natembeya akidai viongozi wa serikali wamekuwa wakipora hela na kuendelea na shughuli zao kama kawaida.
“Sasa naelewa kwa nini wanamlenga Natembeya. Ni kwa sababu yeye ni mwanasiasa mwenye msimamo mkali na kigogo wa siasa za Magharibi,” akasema Bw Wajackoya.
Wawili hao waliahidi kuongoza mikutano ya kuondoa Kenya Kwanza Magharibi mwa nchi wakisema uongozi wa sasa haujanufaisha eneo hilo kivyovyote kimaendeleo.