Natembeya asema anasuka ‘kitu’ na Sifuna
GAVANA wa Trans Nzoia, George Natembeya, na Seneta wa Nairobi, Edwin Sifuna wamechangamsha wafuasi wake wa kuandaa mkutano wa faragha na kutangaza kuwa wako katika mwelekeo sahihi hatua inayochukuliwa wanasuka ushirikiano kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.
Kupitia taarifa aliyochapishwa kwenye ukurasa wake rasmi wa Facebook Alhamisi, Januari 29, 2026, Gavana Natembeya alitoa picha na kauli iliyoonyesha akijadiliana na seneta huyo wa Nairobi.
Katika ujumbe huo, Natembeya aliwahakikishia wafuasi wake kuwa yeye na Sifuna wako imara kisiasa na wako kwenye mwelekeo sahihi.
Ingawa Sifuna hakutoa maelezo yoyote kuhusu mkutano huo katika anwani zake za mitandao ya kijamii, ulijiri miezi kadhaa baada yake kutangaza hadharani kuwa yuko tayari kufanya kazi na gavana huyo wa Trans Nzoia.
Mkutano huo pia ulifanyika takriban miezi sita baada ya Seneta Sifuna kusema wazi kuwa hakuna mtu anayeweza kuzuia ushirikiano wake au mawasiliano yake ya kisiasa na Gavana Natembeya.
Akizungumza na wakazi wa Saboti Jumapili, Agosti 3, 2025, wakati wa hafla ya uwezeshaji wa wanawake iliyoandaliwa na Mbunge wa Saboti, Caleb Amisi, Bw Sifuna alisema alikuwa tayari amemfahamisha Natembeya kuhusu uwepo wake Trans Nzoia na kusisitiza kuwa yuko tayari kushirikiana na kiongozi yeyote anayeunga mkono ajenda ya kisiasa inayowiana na yake.
Kwa mujibu wa Sifuna, Bw Natembeya ana maono yanayofanana na yake ya kuhakikisha kuwa utawala wa sasa hauchaguliwi tena kwa muhula wa pili. Alisema kuwa mradi Natembeya ataendelea kujitolea kwa lengo hilo, hana kizuizi chochote cha kushirikiana naye kisiasa.
“Nilimpigia gavana simu akajua niko hapa Trans Nzoia. Watu wote watakaotusaidia kumpeleka Ruto nyumbani ni washirika wetu. Kumtoa Ruto madarakani ni mradi wa kitaifa. Ndugu yangu Natembeya, hakuna mtu atakayenizuia kuzungumza na wewe,” alisema Sifuna.