Habari

Nyama: Kenya yapoteza Sh250m kila wiki kutokana na vita Mashariki ya Kati

Na EDWIN MUTAI April 4th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KENYA inapoteza takriban Sh250 milioni kila wiki kutokana na kuvurugika kwa mauzo ya mifugo na nyama nje ya nchi kufuatia vita vinavyoendelea kati ya Amerika, Israeli na Iran, hali ambayo imeibua wasiwasi mkubwa katika sekta ya mifugo.

Kulingana na Waziri wa Fedha John Mbadi, hasara hiyo tayari imefikia zaidi ya Sh1 bilioni ndani ya mwezi mmoja uliopita, huku masoko muhimu ya nchi za Ghuba yakidorora.

Eneo la soko chini ya Gulf Cooperation Council (GCC) linachangia asilimia 85 ya mauzo ya mifugo na karibu asilimia 69 ya mauzo ya nyama ya Kenya nje ya nchi.

“Vurugu katika masoko haya zimesababisha hasara ya takriban Sh250 milioni kila wiki, huku vichinjio sita vilivyoidhinishwa vikifanya kazi kwa kiwango cha chini sana,” alisema Mbadi alipowasilisha ripoti mbele ya Kamati ya Bunge ya Fedha na Mipango ya Kitaifa.

Aliongeza kuwa hali hiyo imeathiri pia soko la ndani, ambapo kukosekana kwa masoko ya nje kumesababisha mifugo ya ziada, na hivyo kushusha bei kwa wafugaji mashinani, hasa katika jamii za wafugaji wa kuhamahama.

“Mapato ya wafugaji yamepungua kwa kiasi kikubwa, na hii imeathiri maisha ya maelfu ya familia zinazotegemea sekta hii,” alionya.

Mbali na kushuka kwa bei, sekta hiyo pia inapoteza ajira katika mfumo mzima wa uzalishaji, ikiwemo katika vichinjio, usafirishaji na usindikaji wa nyama.Ili kukabiliana na changamoto hiyo, serikali inapendekeza hatua za haraka zikiwemo kutafuta masoko mbadala katika Umoja wa Ulaya, China, Amerika na mataifa mengine ya Afrika.

Pia imependekeza kujadili njia mbadala za usafirishaji wa mizigo ili kuendeleza mauzo hata kwa kiwango kidogo.

Katika muda wa kati, Mbadi alisisitiza umuhimu wa kuwekeza katika miundombinu ya uhifadhi wa baridi ili kupunguza kutegemea njia chache za usafirishaji na masoko maalum.

Wakati huo huo, Wizara ya Maendeleo ya Mifugo imekiri kuwa Kenya bado haijanufaika kikamilifu na soko la Ghuba licha ya kutia saini makubaliano ya kibiashara na Milki ya Kiarabu.

Serikali inalenga kubuni mkakati mpya wa kukuza mauzo ya nyama, hasa bidhaa zilizoidhinishwa kwa viwango vya halal zinazohitajika sana Mashariki ya Kati.

Kenya ina takriban ng’ombe milioni 22, kondoo milioni 23, mbuzi milioni 35 na ngamia milioni 4.3, lakini uzalishaji bado haujakidhi mahitaji ya ndani na nje.

Mahitaji ya nyama nyekundu nchini yanakadiriwa kuwa tani 800,000 kwa mwaka, ilhali uzalishaji ni takriban tani 607,000 pekee.

Changamoto nyingine zinazoikumba sekta hii ni pamoja na ukosefu wa mipango thabiti ya ufugaji, gharama kubwa ya lishe ya mifugo, uhaba wa maghala ya baridi, pamoja na gharama ya juu ya usafirishaji wa angani.