Habari

OneTam: Ndoana ya Sifuna yanasa Maraga 2027 ikikaribia

Na RUTH MBULA July 4th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

ALIYEKUWA Jaji Mkuu David Maraga ameongeza nguvu mpya kambi ya Linda Mwananchi baada ya kuungana na viongozi wake katika juhudi za kuimarisha umoja wa upinzani kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.
Bw Maraga alisema yuko tayari kushirikiana na kundi hilo linaloongozwa na Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna, Gavana wa Siaya James Orengo, Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino na Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi, kwa lengo la kuhakikisha Rais William Ruto anaondolewa mamlakani katika uchaguzi ujao.
Kauli hiyo ilitolewa Ijumaa alipohudhuria mikutano ya kisiasa katika mji wa Kisii, Keumbu na Keroka, baada ya kufanya mazungumzo na baadhi ya viongozi wa kundi hilo mapema Alhamisi.
Akizungumza katika mkutano wa kuwawezesha wanawake uliofanyika katika Hoteli ya Monarch, eneo la Mosocho, Kaunti ya Kisii, Bw Maraga alisema wananchi wamemtaka ashirikiane na viongozi wenye maono sawa na yake ili kurejesha Kenya katika mkondo unaofaa.
“Wananchi wanasema kinachoiangamiza nchi yetu ni wizi wa mali ya umma na wanataka mali hiyo irejeshwe. Waliniambia, ‘CJ, nenda ukaungane na wenzako ili tuwe na umoja na kurejesha nchi yetu mahali panapostahili.’ Ndiyo maana nimejiunga na Linda Mwananchi. Tunataka kufanya kazi na wote wanaotaka Kenya ipige hatua,” alisema.
 Bw Maraga, ambaye amekuwa akizuru maeneo mbalimbali nchini kama kiongozi wa chama cha United Green Movement (UGM), alimshambulia Rais Ruto kwa madai ya ukiukaji wa haki za binadamu.
Alidai kuwa serikali imekuwa ikihusishwa na mauaji ya vijana na baadaye kutoa fidia kwa familia zao.
“Hawawezi kuendelea kuwaua watoto wetu halafu wawape wazazi wao Sh1 milioni kama fidia. Kenya haiwezi kuendelea kwa njia hii. Itakuwa janga kubwa ikiwa Ruto atarejea mamlakani 2027. Hatutakuwa na nchi kama atachaguliwa tena. Lazima tuungane na kuiondoa serikali hii madarakani,” alisema.
Kwa upande wake, Seneta Sifuna alisema Linda Mwananchi haitatumika kugawanya kura za upinzani, akisisitiza kuwa kundi hilo litaungana na muungano mpana wa upinzani ili kuongeza nafasi za ushindi.
“Kuna wanaodhani kwamba ninashinikizwa kugombea urais peke yangu ili kugawanya kura na kumwezesha Ruto kushinda. Hilo halitafanyika. Tutazungumza na Dkt Fred Matiang’i na kuhakikisha tunashirikiana naye pamoja na viongozi wengine wa upinzani ili kuunda kikosi kitakachoshinda uchaguzi,” alisema.
Sifuna aliongeza kuwa ingawa Linda Mwananchi ina uwezo wa kushinda uchaguzi peke yake, umoja wa upinzani ndio njia bora ya kutimiza matakwa ya wananchi.
“Wananchi wanataka Ruto aondoke mapema iwezekanavyo. Tutakaa pamoja na kuunda muungano imara utakaoleta ushindi,” alisema.
Gavana Orengo alisema sababu kuu za kupinga serikali ya Kenya Kwanza ni madai ya kuibwa kwa ushindi wa aliyekuwa Waziri Mkuu Raila Odinga katika uchaguzi wa 2022, pamoja na visa vya mauaji ya kiholela, utekaji nyara na kukamatwa kwa watu bila kufuata sheria.
Aliwahakikishia vijana wa Gusii kuwa yuko tayari kuwapa huduma za kisheria bila malipo endapo watakumbwa na matatizo kutokana na shughuli za kisiasa.
“Tutafanya kazi na Dkt Matiang’i na viongozi wengine wa upinzani ili kuhakikisha serikali ya Ruto inaondoka madarakani,” alisema.
Naye Babu Owino alishutumu serikali kwa kile alichodai kuwa ni kuendeleza ufisadi unaozorotesha utoaji wa huduma muhimu kwa wananchi.
“Kila shilingi inayoibwa ni darasa ambalo halijajengwa, kitanda cha hospitali kisichonunuliwa, dawa ambazo wagonjwa hawatapokea na barabara ambayo haitajengwa. Wakenya wamechoshwa na hali hii,” alisema.
Ingawa Dkt Matiang’i hakuhudhuria mikutano hiyo, viongozi wote waliohutubia umma walisisitiza kuwa wako tayari kushirikiana naye katika kuunda muungano mpana wa upinzani kabla ya uchaguzi mkuu wa 2027.
 Miongoni mwa viongozi waliohudhuria ni wabunge Obadiah Barongo (Bomachoge Borabu), Caroli Omondi (Suba Kusini), Joshua Kimilu (Kaiti), Clive Gisairo (Kitutu Masaba), Majimbo Kalasinga (Kabuchai), Patrick Makau (Mavoko), mwenyeji Anthony Kibagendi (Kitutu Chache Kusini), pamoja na aliyekuwa Rais wa Chama cha Wanasheria nchini (LSK), Faith Odhiambo.